1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUkraine

Trump akwaruzana tena na Zelensky

24 Aprili 2025

Rais Donald Trump wa Marekani jana Jumatano amejikuta kwenye mvutano kwa mara nyingine na Rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine kuhusiana na juhudi za kumaliza vita vya nchini Ukraine vilivyodumu kwa miaka mitatu sasa.

Marekani | Rais Donald Trump
Rais Donald Trump amemshutumu Rais Volodymyr Zelensky kwa kurudisha nyuma juhudi za amani nchini UkrainePicha: Nathan Howard/REUTERS

Trump aidha amemshutumu Zelensky kwa kukataa kutambua udhibiti wa Urusi kwenye jimbo la Crimea. 

Mjini Washington, Rais Donald Trump wa Marekani amesema anaamini amefikia makubaliano na marais wote wawili wa Ukraine Volodymyr Zelensky na Vladimir Putin wa Urusi ya kuvimaliza vita vnavyoendelea nchini Ukraine.

Hata hivyo amekiri alipozungumza na waandishi wa habari katika ikulu ya White House kwamba, imekuwa ngumu sana kwake kuzungumza na Zelensky, tofauti na alivyotarajia.

Maafisa wengine wa Marekani walisema mapema Jumatano kwamba bado hakujafikiwa makubaliano na Marekani inaweza kujiondoa kwenye mazungumzo ya amani ikiwa hakutapigwa hatua za haraka, Baadae Trump alisema akiwa kwenye ofisi yake ya Oval kwamba anadhani Urusi iko tayari na wamefikia makubaliano, lakini bado hawajakubaliana na Zelensky.

Soma pia: JD Vance azitaka Urusi na Ukraine kufikia makubaliano

Alisema "Kila kitu kiko sawa. Ninachotaka mimi ni kuona vita vinamalizika. Sitojali kama wote watafurahia, ama pande zote zimekubaliana. Siupendelei upande wowote. Siaki kupendelea upande wowote. Ninataka kuona kunafikiwa makubaliano. Ninataka kuokoa maisha ya watu."

Marekani imetishia kujitoa kwenye mazungumzo ya amani nchini Ukraine ikiwa hatua hazitapigwa Picha: Geert Vanden Wijngaert/ AP Photo/picture alliance | Al Drago/UPI Photo/IMAGO

Na alipoulizwa kuhusiana na pendekezo la Marekani kwa Ukraine la kuitambua haki ya Urusi kuimiliki Rasi ya Crimea, Trump hakutaka kulizungumzia moja kwa moja, bali aliendelea tu kusisitiza haipendelei ama Urusi au Ukraine, bali anachokitaka ni vita kumalizika. Crimea ni eneo linalotambulika kimataifa kuwa ni sehemu ya Ukraine na Kyiv inasema inaitaka rasi hiyo ya Bahari Nyeusi. Urusi ililichukua eneo hilo mwaka 2014.

Kwa ujumla matamshi ya Trump yakatofautiana na yale yaliyotolewa awali na maafisa wa ngazi za juu kwenye serikali yake. Masaa machache kabla ya kuzungumza na waandishi hao wa habari, msemaji wa White House Karoline Leavitt aliwaambia waandishi wa habari kwamba Trump amechoshwa na kasi ya mazungumzo na kwamba Zelensky anaonekana kuchukua mwelekeo mbaya.

Soma pia:Kremlin: Mazungumzo na Kiev yatafanyika vikwazo vikiondolewa

Zelensyk akatisha ziara yake Afrika Kusini kufuatia mashambulizi ya Urusi

Mjini Johannesburg Rais Zelensky amesema analazimika kukatisha ziara yake nchini Afrika Kusini na kurejea nyumbani baada ya Urusi kuishambulia Kyiv usiku wa kuamkia Alhamisi.

Zelensky aliwasili Jumatano usiku nchini humo kwa ziara ya kikazi, katikati ya tuhuma hizi mpya za Trump kwamba kiongozi huyo alikuwa akiviendeleza vita kutokana na kukataa kutambua haki ya Urusi kulimiliki eneo hilo la Crimea, kipengele ambacho ni muhimu kwenye makubaliano ya amani.

Mashambulizi ya Urusi nchini Ukraine yameendelea kusababisha vifo, maeneo na miundombinu nchini humoPicha: Ukrainian Emergency Service/UPI Photo/Newscom/picture alliance

Lakini akiwa safarini, Urusi imefanya mashambulizi makubwa ya droni na makombora mjini Kyiv usiku wa kuamkia leo na kuwaua watu 9 na kuwajeruhi wengine zaidi ya 60, miongoni mwao watoto 6, hii ikiwa ni kulingana na mamlaka za Ukraine.

Soma pia:Vikosi vya Urusi vyashambulia Odesa kwa droni

Vikosi vya uokozi na dharura vimesema mashambulizi hayo yalisababisha moto kuwaka kwenye maeneo karibu 40 na vipande vya vyuma vilianguka na kuharibu magari. Mji wa Kharkiv ambao ni wa pili kwa ukubwa nchini Ukraine, nao ulishambuliwa, amesema meya ya mji huo.

Wakati haya yakiendelea, kutoka mjini Washington taarifa zinasema Katibu Mkuu wa NATO Mark Rutte anakwenda mjini humo hii leo kuzungumza na maafisa waandamizi wa serikali ya Marekani, miongoni mwao ni Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio na Mshauri wa Usalama wa Taifa Mike Waltz, na mazungumzo yao yatajikita kwenye juhudi za kuvimaliza vita nchini Ukraine, hii ikiwa ni kulingana na NATO na Wizara ya mambo ya Nje ya Marekani.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW