1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Kiir amfuta kazi waziri wake wa mambo ya nje

9 Machi 2023

Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir, amemfuta kazi waziri wake wa mambo ya nje Mayiik Ayii, wiki moja baada ya kufutwa kazi kwa waziri wa ulinzi Angelina Teny na wa masuala ya ndani Mahmoud Solomon bila ya maelezo yoyote.

Salva Kiir Mayardit | sudanesischer Präsident
Picha: Samir Bol/ZUMAPRESS/picture alliance

Haya yamesemwa na msemaji wa rais Kiir, Lily Martin Manyiel. Manyiel amesema ni hali ya kawaida kwamba watu wanaweza kupumzishwa na nyadhifa zao kupatiwa watu wengine. Ayii alikuwa mshirika wa karibu wa Kiir na awali alihudumu kama waziri katika ofisi ya rais.

Kiir amfuta uwaziri mke wa Machar

Haikubainika mara moja iwapo kufutwa kazi kwa Ayii kulihusishwa na kufutwa kazi kwa Teny na Solomon ambako kumetishia kuharibu mkataba tete wa amani na kiongozi rasmi wa upinzani makamu wa rais wa kwanza Riek Machar.

Machar ameilaani hatua hiyo na kutoa wito kwa Kiir kumrejesha Teny ambaye ni mkewe katika wadhifa wake lakini hakutishia kujiondoa katika mkataba wa amani.