1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Samia ataja baraza la mawaziri, lina wizara mbili mpya

17 Novemba 2025

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ametangaza baraza jipya la mawaziri likiwa na mabadiliko makubwa ya kiwizara sambamba na sura mpya za mawaziri walioteuliwa kuongoza wizara hizo, akiongeza wizara mpya mbili.

Tanzania Dodoma 2025 | Rais Samia Suluhu Hassan akizindua Bunge la 13
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiwahutubia wabunge katika Bunge la Tanzania wakati wa uzinduzi rasmi wa Bunge la 13 mjini Dodoma mnamo Novemba 14, 2025.Picha: AFP

Rais Samia Suluhu Hassan ametangaza baraza  jipya la Mawaziri, likiwa na wizara mpya  mbili, Wizara ya kazi, Ajira na Mahusiano na Wizara ya Vijana.

Hatua ya kuundwa kwa wizara hizi imekuja ikiwa siku chache baada ya rais kulihutubia bunge Novemba 14 akitoa ahadi ya kuunda wizara kamili ya Vijana itakayosikiliza na kufanyia kazi changamoto za vijana ambayo itakuwa chini ya ofisi ya rais.

Akizungumza na wanahabari leo Ikulu ya Chamwino, Dodoma, Rais Samia amesema amefanya marekebisho kidogo wizara ya kazi na ajira na kuongeza kipengele cha mahusiano ambacho kitafanya kazi na makundi mbalimbali ili kujenga mahusiano mazuri.

Nani kaingia?

Waliochaguliwa kushika nafasi katika wizara hizo mpya ni Joel Arthur Nanauka, Waziri wa Maendeleo ya Vijana na Deus Clement Sangu, Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo.

Paul Christian Makonda, ateuliwa kuwa Naibu waziri wa Pili wa Wizara ya habari Utamaduni, Sanaa na MichezoPicha: DW/S. Khamis

Sura mpya zilizoingia kwenye baraza la mawaziri ni pamoja na Paul Christian Makonda aliyeteuliwa kuwa Naibu waziri wa Pili, Wizara ya habari Utamaduni, Sanaa na Michezo na Wanu Hafidh Ameir akichaguliwa kuwa Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia na Nanauka ambaye anaongoza Wizara ya Vijana.

Pamoja na sura hizo mpya, wapo mawaziri wa zamani ambao nafasi zao zimezibwa na mawaziri wengine, akiwamo aliyekuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk Dotto Biteko; Hussein Bashe aliyekuwa (Kilimo); Innocent Bashungwa aliyekuwa (Mambo ya Ndani); Jenista Mhagama aliyekuwa (Afya); na Dkt. Seleman Jafo aliyekuwa (Viwanda na Biashara).

Kadhalika Rais Samia amewateua Balozi Khamis Musa Omar, kuwa waziri wa Fedha, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa kimataifa na Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ikiongozwa na Angella Kairuki.

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW