Urusi imewapeleka zaidi ya Wakenya 1,000 kupigana Ukraine
19 Februari 2026
Uchunguzi mwingi wa vyombo vya habari, ukiwemo ule uliochapishwa mapema mwezi huu na AFP, umefichua jinsi Urusi ilivyowashawishi wanaume kutoka nchi za Afrika kwa ahadi za ajira zenye mishahara minono, na badala yake kuwalazimisha kupigana mstari wa mbele nchini Ukraine.
Uchunguzi wa pamoja uliofanywa na Idara ya Kitaifa ya Ujasusi ya Kenya na Kurugenzi ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai, uliowasilishwa bungeni Jumanne, ulisema idadi ya walioajiriwa kutoka nchini humo ni "zaidi ya 1,000" -- ikiwa ni juu zaidi kuliko idadi ya "karibu watu 200" iliyotolewa na mamlaka mwezi Desemba. Kiongozi wa serikali bungeni Kimani Ichung'wah amesema Wakenya huondoka nchini kwa kutumia viza ya watalii ili kujiunga na jeshi la Urusi kupitia Instanbul, Uturuki, pamoja na Umoja wa Falme za Kiarabu.
Lakini alisema kuongezeka kwa utekelezaji wa sheria za mpaka katika uwanja wa ndege wa Nairobi kulimaanisha kuwa waajiriwa pia sasa wanasafiri kwenda nchi zingine za Afrika ili kuepuka kugunduliwa. Ichung'wah aliongeza kuwa mashirika ya ajira yasiyo na kibali nchini Kenya "yanashirikiana na wafanyakazi wafisadi wa uwanja wa ndege". Takribani Wakenya 39 wamelazwa hospitalini kwa sasa, 28 hawajulikani waliko na 89 wako vitani.