Romney, Santorum bega kwa bega
7 Machi 2012Gavana wa zamani wa jimbo la Massachusetts Mitt Romney ameshinda majimbo ya Virginia, Vermont, Massachusetts na jimbo muhimu la Ohio, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Marekani, baada ya vituo vya kupigia kura katika majimbo hayo kufungwa , katika mpambano mkali wa kuwania uteuzi kwa tikiti ya chama cha Republican katika uchaguzi wa rais hapo Novemba mwaka huu dhidi ya rais Barack Obama kutoka chama cha Democratic.
Gingrich aambulia
Spika wa zamani wa baraza la wawakilishi nchini Marekani Newt Gingrich , anahitaji ushindi kuweza kurejea katika njia ya kuwania tikiti hiyo ya chama cha Republican , ambapo ameshinda kwa kishindo katika jimbo anakotoka la Georgia, kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Marekani.
Kwa mujibu wa matokeo ya awali , Gingrich amepata asilimia 45 katika jimbo la Georgia, ikilinganishwa na asilimia 26 alizopata Mitt Romney na asilimia 20 kwa seneta wa zamani kutoka jimbo la Pennsylvania Rick Santorum.
Romney mwenye umri wa miaka 64 anamatumaini ya kushinda mengi kati ya majimbo hayo kumi ambayo yamepiga kura jana Jumanne na kuondoa shaka zilizopo kuwa yeye ni mgombea bora kabisa kwa ajili ya uchaguzi wa hapo Novemba mwaka huu dhidi ya Barack Obama.
Kazi bado pevu
Lakini hata baada ya uchaguzi uliofanyika jana Jumanne bado njia ni ndefu katika mpambano huo wa jimbo kwa jimbo wa uteuzi wa chama cha Republican ambapo hatimaye mgombea wa chama hicho atateuliwa.
Mbali na Mitt Romney kupata ushindi wa majimbo matatu muhimu, lakini mgombea mwingine Rick Santorum ameshinda pia katika majimbo matatu muhimu ya Oklahoma ,Tennesseee na Virginia.
Wagombea wanaofuatia nyuma ya Mitt Romney na Rick Santorum, ni Gingrich na Ron Paul , wote wakiwa na matumaini ya kupata sehemu yao ya kura za wajumbe wanaohitajika ili kuweza kupata kuteuliwa.
Obama awatakia heri wagombea
Rais Barack Obama nae ameweka mtazamo wake katika kinyang'anyiro hicho cha chama cha Republican mapema jana Jumanne katika mkutano na waandishi habari katika Ikulu ya Marekani ya White House. Kitu gani unataka kumwambia Romney , Obama aliulizwa saa kadha kabla ya vituo vya uchaguzi kufungwa. Kila la kheri , amesema akitabasamu, na kusababisha kicheko kutoka kwa waandishi habari.
Mwandishi : Sekione Kitojo /dpae/afpe/rtre