1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Afghanistan yawaacha huru wafungwa wa Taliban

Sekione Kitojo
2 Agosti 2020

Serikali ya Afghanistan imewaacha huru wafungwa 317 wa kundi  la Taliban tangu mwanzoni mwa sikukuu ya Eid-al Adha siku ya Ijumaa, ofisi ya baraza la usalama la taifa imesema leo Jumapili (02.08.2020).

Afghanistan - Bagram Gefängnis in Parwan
Picha: picture-alliance/AP/R. Gul

Idadi jumla ya wafungwa wa  kundi la walioachiliwa kutoka  jela nchini  Afghanistan imefikia  wafungwa 4,917, baraza  hilo  limesema.

Wafungwa  hao 317 ni  miongoni mwa  jumla  ya  wafungwa  wengine 500  wa  Taliban  ambao  rais wa  Afghanistan Ashraf Ghani aliamuru waachiliwe  huru siku  ya  Ijumaa kama ishara ya kuonesha nia njema.

Wafungwa wa kundi la Taliban walioachwa huru na serikali wakisafirishwa Picha: picture-alliance/AP Photo/R. Gul

Kundi  la  Taliban bado  halijatoa tamko lolote kuhusiana  na kuachiwa  kwa  kundi  hilo la  hivi  sasa  la  wafungwa.

Hata  hivyo, siku  ya  Ijumaa Ghani  alisema  kuwa  hana "mamlaka" chini  ya  katiba  ya  nchi  hiyo kuwaachilia  huru wafungwa  wengine 400  waliobakia walioko  katika  orodha ya Taliban  ya kuachiwa kwasababu  wamehusika  katika  uhalifu  mkubwa.

Kusitishwa mapigano

Ameongeza  kuwa  karibuni  ataitisha baraza la  mashauriano  la Loya Jirga, baraza kuu  la  wazee wa kikabila , kuamua  hatima yao. Kundi  hilo  la  wanamgambo  limesema  limewaacha  huru wafungwa 1,000 ilioahidi kuwaacha  huru  katika  makubaliano  na  Marekani.

Rais wa Afghanistan Ashraf GhaniPicha: Getty Images/AFP/W. Kohsar

Taliban  wametangaza makubaliano  ya  muda  ya  kusitisha mapigano kwa  muda  wa  siku  tatu wakati  wa  sikukuu  ya  Eid al-Adha kuanzia  Ijumaa iliyopita. Serikali  ilijiunga  na   hatua  hiyo  ya kusitisha  mapigano.

Makubaliano  ya  Taliban na  Marekani  yanasafisha  njia kwa  ajili ya  kuondolewa  majeshi  yote ya  kigeni kutoka  Afghanistan na mabadilishano  ya  wafungwa  kati ya  serikali  ya  Afghanistan na wanamgambo  hao. Pia  yanasafisha njia  kwa  ajili  ya  mazungumzo ya  amani  baina  ya  Waafghanistan.

Mwandishi: Sekione Kitojo / dpae

Mhariri: Tatu Karema  

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW