Sherehe za kutunukiwa zawadi ya Nobel zitaanza hivi punde
10 Desemba 2010Tuzo ya amani ya Nobel anatunukiwa hii leo mpigania demokrasia wa China, Liu Xiaobo, bila ya mwenyewe kuhudhuria sherehe hizo mjini Oslo. Jamhuri ya umma wa China imekosoa uamuzi huo.
Hakuna mtu yeyote wa familia yake anaeshiriki katika sherehe hizo za kutolewa tuzo ya amani ya Nobel zitakazoanza saa mbili kutoka sasa katika mji mkuu wa Norway Oslo.Na pia nchi 20 kati ya 45 zilizoalikwa, ikiwa ni pamoja na Urusi, Iran, Afghanistan na Saudi Arabia haziwakilishwi katika sherehe hizo; zinajibu shinikizo la kidiplomasia la jamhuri ya umma wa China.
Mshindi huyo wa zawadi ya amani ya Nobel, Liu Xiaobo, atawakilishwa na kiti kitupu, picha yake imetundikwa na mojawapo ya risala zake itasomwa na msanii wa kutoka Norway, Liv Ullmann.
Mwenyekiti wa kamati ya amani ya Nobel, Thorbjorn Jagland, anasema:
"Hatuwezi kuzingatia masilahi ya nchi moja moja.Tunatangulitza mbele wasia wa Alfred Nobel tu."
Jamhuri ya umma wa China imelaani vikali uamuzi wa kumtunukia mwanaharakati huyo wa haki za binaadamu, Liu Xiaobo, zawadi hiyo ya amani ya Nobel na wanaharakati wote pamoja na familia zao wanazidi kumulikwa .
"Hii leo kuna kiroja mjini Oslo,nchini Norway-Kesi ya China" ni mojawapo ya vichwa vya maneno vya uhariri wa magazeti yanayomilikiwa na serikali nchini China hii leo.
Hatua za usalama zimeimarishwa mjini Beijing na magari ya polisi yanapiga doria na hasa karibu na nyumba ya Liu , karibu na uwanja wa Tiananmen na ubalozi wa Norway.
Polisi wamewazuwia baadhi ya wanadiplomasia wa Ujerumani kuijongelea nyumba ya Liu ambako mkewe Liu Xia anatumikia kifungo cha nyumbani.
Ripoti zinasema watu kama mia moja hivi wameandamana karibu na makao makuu ya Umoja wa mataifa mjini Beijing.
Katika historia ya miaka 109 ya tuzo ya amani ya Nobel, hii ni mara ya pili kwa tuzo hiyo kushindwa kukabidhiwa mshindi au mwakilishi wake. Katika Ujerumani ya zamani ya wanazi, mpigania amani, Carl von Ossietzky, alizuwiliwa kwenda kupokea zawadi yake mwaka 1936 kwa sababu alikuwa wakati ule akishikiliwa katika kambi ya mateso.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir,afp,reuters,dpa
Mpitiaji: Miraji Othman