Sherehe za Muungano wa Ujerumani
3 Oktoba 2010Usiku ule umati mkubwa ukipiga fashifashi za kushangiria, macho ya watu wengine wengi yalikuwa yanatiririka machozi. Hawa walikuwa ni mashahidi wa mwenendo wa historia wa namna ambavyo Wajerumani walifanikiwa kwa mara ya kwanza katika historia ya Ulaya Mashariki kufanya mapinduzi ya amani. Bila ya kutumia silaha wala kumuumiza mtu, siku ya tarehe 3 Oktoba 1990 Wajerumani ya Mashariki wakaifanya serikali yao ya kisoshalisti kusalimu amri na kujiunga na wenzao wa Ujerumani ya Magharibi, na hivyo taifa hili likarudi tena kuwa moja kama ambavyo lilikuwa kabla ya kugawiwa.
Katika usiku huu wa kihistoria, Rais wa Shirikisho la Ujerumani, Richard von Weizsäcker aliitaja dhamira ya muda mrefu ya watu wa Ujerumani kwamba sio tu ni kuziunganisha pande zake mbili zilizokuwa zimetenganishwa, bali ni kuiunganisha Ulaya nzima. Alikuwa anazungumzia Umoja wa Ulaya. "Sisi Wajerumani tunaujuwa wajibu wetu na tunataka kuiona Ulaya nzima ikija pamoja na ikiishi kwa amani," alisema katika usiku huo muda mchache kabla ya fashifashi hazijaanza.
Hapakuwa na Kulala
Msimamizi Mkuu wa Ofisi ya Kansela wa wakati huo, Rudolf Seiters, alikuwa amefanya kazi ngumu kabla ya usiku huu. Akiwa mtu wa karibu wa Kansela wa Helmut Kohl, alikuwa kwenye pirika pirika nyingi miezi miwili mizima. Na usiku mmoja kabla ya usiku huu wa sherehe, anakumbuka kwamba serikali nzima ilikuwapo Berlin na, kwa hivyo, hakuweza kabisa kufikiria kwenda kitandani kulala.
"Nilikuwa na mengi ya kuyafikiria na kuyafanya kwa wakati mmoja. Vyumba vya wanadiplomasia, mkutano na balozi wetu wa Prag Hans-Dietrich Genscher, anwani yangu baada ya ukuta kuanguka, na bila ya shaka hotuba muhimu ya Helmut Kohl mbele ya kanisa la Wanawake mjini Dresden."
Siku 323 za Kusisimua
Kutoka kuanguka kwa ukuta wa Berlin hadi kufikira tarehe 3 Oktoba 1990, zilikuwa zimepita siku 323. Kwa wanasiasa wa pande zote mbili za Ujerumani, hizo zilikuwa siku za kupambana na hali ya mkanganyiko na za kufanya maamuzi ya magumu na ya maana. Kwa upande wa Ujerumani Mashariki, kulikuwa kumefanyika uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia kwenye mwezi Machi 1990, ambao ulishuhudia wanasiasa wengi wahafidhina wakiangushwa. Kwenye uchumi, thamani ya sarafu ya Deutsche Mark ilikuwa imeporomoka sana. Ulaya ilikuwa inashuhudia na inaunga mkono mageuzi yanayotokea katika nchi mbalimbali za Mashariki, na juu ya yote uhuru wa watu kwenda watakako ndani ya Bara la Ulaya ukawa unapigiwa chapuo.
Kupitia kile kinajuilikana kama "Glasnost na Perestroika" yaani Uwazi na Mwanzo Mpya, ambao ulichochewa na mabadiliko ya kusambaratika kwa Muungano wa Kisovieti, mataifa mengi katika Ulaya ya Mashariki yakaingia kwenye maandamano ya kudai mabadiliko. Rudolf Seiters anakumbuka: "Ringi la mabadiliko lilikuwa linazunguka kwa tahadhari lakini kwa haraka, si kuelekea Moscow tu, bali hata kwenye nchi zote za Ulaya ya Magharibi. Mambo yalikuwa yanabadilika."
Dirisha la Muungano
Matukio mengine kadhaa yaliyobadilisha siasa za kilimwengu yalikuwa yanatokezea wakati huo ulimwenguni, sambamba na hili la kuungana tena kwa Ujerumani. Kwa mfano, katika Ghuba, Irak ilikuwa imeivamia Kuwait na kuitangaza kuwa ni sehemu ya nchi yake, na katika Umoja wa Kisovieti, vifaru vya Jeshi Jekundu la Urusi vilikuwa vimeizunguka ikulu ya Kremlin kumlazimisha Gorbachev ajiuzulu. Hata hivyo, kutokana na nafasi yake, ulimwengu haukuacha kuuangalia Muungano wa Ujerumani.
Dhamira ya Wajerumani kuungana tena ilipokelewa kwa shaka na mataifa mengine makubwa ya Ulaya. Kulikuwa na khofu ya kuwa na Ujerumani yenye nguvu katikati ya Bara la Ulaya. kwa mfano, Waziri Mkuu wa wakati huo wa Uingereza, Margaret Thatcher, alijaribu kuchukua juhudi za makusudi kuzuia muungano huu, na Rais wa wakati huo wa Ufaransa, Francois Mitterand hakulipendelea wazo la Ujerumani iliyoungana.
Umoja wa Kisovieti ulikuwa inatiwa khofu na maendeleo ya haraka kwenye siasa za Ulaya Magharibi. Wasiwasi wa dola hiyo ulikuwa ni kupotea kwa ushawishi wake katika mataifa yaliyokuwa kwenye kambi ya Warsaw na wakati huo huo mahasimu wake wa NATO wakija juu na mfumo wa uchumi wa kibepari ukiingia kwa kasi.
Msingi wa Muungano wa Ujerumani
Kwa hivyo, chimbuko hasa la Muungano wa Ujerumani ni amani na maendeleo. Baada ya kutoka katka vita vikuu mara mbili na baada ya kuvunjwa kabisa na kugawiwa kutokana na vita hivyo, Wajerumani walikuwa wamejifunza kwamba ni amani tu ndiyo itakayowaleta pamoja na kuijenga nchi yao.
Mwandishi: Hellfeld,Mathias von/Khelef Mohammed
Mhariri: Abdulrahman Mohamed