1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaRwanda

Rwanda yatishia kuondoa wanajeshi wake Cabo Delgado

17 Aprili 2026

Mustakabali wa operesheni ya kijeshi ya Rwanda dhidi ya ugaidi Cabo Delgado uko mashakani. Kigali inadai malipo au manufaa kwa juhudi zake, hali inayoiweka Ulaya katika mtanziko wa kimkakati.

Msumbiji Palma 2023 | Vikosi vya Rwanda vya kupambana na ugaidi na polisi wanapiga doria
Rwanda ina takribani wanajeshi 4000 katika jimbo la Cabo Delgado, wanaohakikisha usalama wa raia na miradi ya uwekezaji katika sekta ya gesiPicha: Cyrile Ndegeya/Anadolu/picture alliance

Rais wa Rwanda Paul Kagame anatishia kuondoa wanajeshi wake kuanzia Mei kutoka jimbo la mgogoro la Cabo Delgado kaskazini mwa Msumbiji, na kwa kufanya hivyo anaiweka hasa Ulaya chini ya shinikizo.

Operesheni dhidi ya waasi wa Kiislamu inaweza kumalizika hivi karibuni ikiwa Umoja wa Ulaya hautatoa ahadi ya uhakika ya ufadhili. Chanzo ni ripoti zinazoeleza kuwa Brussels inaweza kusitisha msaada wake kwa operesheni hiyo. Umoja wa Ulaya umechangia euro milioni 40, ambazo inadaiwa ni chini ya humusi ya gharama zote za Rwanda.

Ni gharama gani hasa za operesheni ya kijeshi ya Rwanda?

Kiwango halisi cha gharama hizo bado kinabishaniwa. Mtaalamu wa usalama kutoka Msumbiji, Borges Nhamirre wa taasisi ya utafiti wa usalama, anaeleza katika mahojiano na DW kuwa takwimu zilizowasilishwa na Kigali ni vigumu kuthibitishwa.

Rwanda, kwa mfano, huhesabu gharama za usafiri kupitia shirika la ndege la serikali RwandAir—lakini "hakuna anayejua kama gharama hizo zilitokea kwa kiwango hicho.” Inawezekana hivyo kuwa gharama zote zimeonyeshwa kuwa kubwa zaidi kuliko zilivyo kwa kweli, anasema mtaalamu huyo anayefuatilia hali ya usalama Cabo Delgado.

Wanajeshi wa Rwanda na msumbiji wakiwa katika doria ya pamoja katika mji wa Palma, uliko Cabo Delgado.Picha: Cyrile Ndegeya/Anadolu/picture alliance

Ulaya inahitaji gesi ya Msumbiji na usalama wa Rwanda

Kwa Msumbiji, kuondoka kwa wanajeshi kungekuwa mshtuko wa kiusalama—kwa Ulaya ni hatari ya kijiografia. "Zaidi ya yote, Umoja wa Ulaya una maslahi yake katika uthabiti wa maeneo ya gesi,” anasisitiza Nhamirre. Wawekezaji wakubwa wanatoka Ufaransa, Italia na nchi nyingine za Ulaya. Usafirishaji wa kwanza tayari umefika Ulaya.

Hata Rwanda yenyewe huenda haina nia ya kuondoa wanajeshi wake haraka, anachambua Nhamirre. Mengi yako hatarini kwa Kigali. "Kama wataondoka sasa, haitakuwa vizuri kwa maslahi mengi ya kibiashara ya Rwanda.” Ushiriki wa Rwanda umedumu kwa muda mrefu.

Kampuni za Rwanda zinanufaika na zabuni katika eneo hilo. Faida zinazotarajiwa zinahusiana moja kwa moja na maendeleo ya miradi ya gesi ambayo bado inaanza polepole. Pia makampuni binafsi ya usalama ya Rwanda yanatarajia kupata zabuni kutoka kwa kampuni za kimataifa zinazowekeza huko.

Kwa hiyo, mwisho wa ghafla wa operesheni unaonekana kuwa hauwezekani, anasema Nhamirre. "Hali inayowezekana zaidi ni kwamba wanajeshi wa Rwanda wataendelea kubaki huko kwa namna moja au nyingine,” anasema mchambuzi huyo.

Wanajeshi wa Rwanda si rahisi kubadilishwa

Tangu mwaka 2021, wanajeshi wa Rwanda wamekuwa wakilinda eneo hilo kwa ombi la serikali ya Msumbiji. Hii imeruhusu miradi mikubwa ya nishati kuanza tena, ambayo ilikuwa imesimamishwa kutokana na mashambulizi ya kigaidi. Leo hii zaidi ya wanajeshi 4000 wako kazini.

Faida yao kubwa ni uzoefu na mitandao ya ndani. "Wanyarwanda sasa wana kumbukumbu ya kitaasisi,” anasema Nhamirre. Ubadilishaji wa haraka hauwezekani. Vikosi vipya vingehitaji kujifunza mazingira magumu—kupambana na waasi wanaojificha miongoni mwa wavuvi au wakulima.

Jeshi la Msumbiji ladhibiti mji wa Mocimboa da Praia

01:36

This browser does not support the video element.

Kisiasa, Kigali inakabiliwa na shinikizo linaloongezeka. Vikwazo vya Marekani na Umoja wa Ulaya kutokana na jukumu la Rwanda katika mgogoro wa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo vinafanya iwe vigumu kuendeleza ufadhili. Rwanda inakanusha kuunga mkono waasi wa M23, lakini waangalizi huru kama Umoja wa Mataifa wametoa ushahidi mara kadhaa.

Kwa Nhamirre, hili ni zaidi ya tatizo la kisiasa: "Inazalisha mkanganyiko mkubwa.” Kwa sababu Umoja wa Ulaya unaunga mkono operesheni ya wanajeshi wa Rwanda Cabo Delgado huku ukipinga kisiasa hatua zao mashariki mwa Kongo. Kuna "hatari kubwa” kwamba fedha za Ulaya zinaweza kuelekezwa bila kukusudia katika migogoro yote miwili.

Mjadala wenye utata ndani ya taasisi za Umoja wa Ulaya

Katika Bunge la Ulaya na taasisi nyingine, mjadala huu unaendelea kwa mvutano. Mbunge wa Ureno katika Bunge la Ulaya, Hélder Sousa Silva, anaonya dhidi ya maamuzi ya haraka. Kusitishwa kwa ufadhili wa operesheni ya Rwanda Cabo Delgado kungekuwa jambo "kubwa na hakupaswi kupuuzwa.” Operesheni hiyo inapaswa kutenganishwa na jukumu la Rwanda Kongo. "Hapa ni kuhusu usalama wa Cabo Delgado na uthabiti wa Msumbiji.”

Hata hivyo, anakubali kuwa suala hilo ni nyeti kisiasa. Vikwazo dhidi ya Rwanda vinafanya hali kuwa ngumu kwa nchi wanachama. Umoja wa Ulaya una maslahi makubwa katika msaada wa wanajeshi wa Rwanda Cabo Delgado. Gharama kwa Ulaya ni ndogo: "Swali halikuwa la rasilimali bali la uamuzi wa kisiasa wa pamoja.”

Katika Picha hii ya Oktoba 2025, Umoja wa Ulaya ulikuwa katika kikao kilichoharakisha uidhinishwaji wa msaada wa EU kwa ajili ya Cabo DelgadoPicha: Delfim Anacleto/DW

Ulaya lazima ibaki kuwa nguvu ya kisiasa na kiuchumi katika eneo hilo. Kujiondoa kutakuwa na athari kubwa: "Ikiwa Ulaya itaondoka, wengine wenye nia tata watachukua nafasi hiyo.”

Cabo Delgado: hali bado ni tete

Kwa Msumbiji, hali bado ni dhaifu. Vikosi vya ndani bado haviwezi kudhibiti eneo hilo peke yao, anasema Nhamirre. "Wakati huo huo, mgogoro unaonyesha mipaka ya mbinu inayotegemea zaidi ulinzi wa kijeshi wa miundombinu. Sababu za vurugu—umasikini, kutengwa na ukosefu wa fursa—bado zipo.”

Kwa hivyo, tishio la Rwanda linaonekana kama mbinu ya shinikizo. Kigali inaashiria: usalama haupatikani bila malipo. Kwa Ulaya, swali ni kama iko tayari kulipa gharama hiyo.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW