Siku ya Wakatoliki wa Ujerumani yaadhimishwa
16 Mei 2012Hii ni mara ya 98 kwa siku ya wakatoliki kuadhimishwa hapa Ujerumani. Mwaka huu maadhimisho hayo yanafanyika katika mji wa Mannheim uliopo Kusini Magharibi mwa nchi hii, katika jimbo la Baden Württemberg. Watu wapatao 33.00 wamejiandikisha kwa ajili ya kuhudhuria maadhimisho ya siku ya wakatoliki hadi Jumapili, huku wengine 30.000 wakitarajiwa kushiriki bila ya kujiandikisha. Takriban misa 80 zitafanyika kuanzia leo hadi Jumapili, siku ambayo maadhimisho haya yatafikia mwisho.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa siku ya wakatoliki, rais wa kamati kuu ya wakatoliki wa Ujerumani, Alois Glück, alionya kuwa kanisa ni lazima lizungumze juu ya masuala muhimu katika jamii, na si kuchangia tu katika mada zisizo na utata.
Kanisa latakiwa kufanya mabadiliko ya sera
Akimuunga mkono, waziri mkuu wa Jimbo la Baden Würtemberg, Winfried Kretschmann, naye aliwataka waumini wazungumzie mambo yaliyopo katika jamii, hata kama yatawachukiza baadhi ya watu na pia wajihusishe katika masuala ya siasa.
Msemaji wa kundi moja la wanaharakati wa kikatoliki, Bw. Christian Weisner, alitoa malalamiko juu ya kutokuwepo kwa mabadiliko ya sera katika kanisa lake. Akizungumza na kituo cha televisheni cha SWR cha hapa Ujerumani, Weisner alieleza kuwa kashfa za unyanyasaji wa kijinsia hadi leo hazijaongelewa wazi wazi na akawalaumu pia maaskofu wa hapa Ujerumani kwa kusita kuzungumzia suala kama hilo.
Nayo jumuiya ya waumini wa kikatoliki imetaka pawepo na mabadiliko ya sera katika kanisa. Jumuiya hiyo imesema kuwa zipo tofauti kubwa kati ya mafundisho ya kanisa na uhalisi wa maisha ya kila siku ya wakatoliki wengi. Miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa ni kufanyiwa marekebisho sheria za talaka na ndoa za watu wa madhehebu tofauti.
Mwandishi: Elizabeth Shoo/epd/dpa/KNA
Mhariri: Othman Miraji