1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Solskjaer kuimarisha kikosi cha ManU

Sekione Kitojo
17 Agosti 2020

Msisimko umezidi kuongezeka katika michuano ya Champions League barani Ulaya na Ligi ya Europa msimu huu

UEFA Europa League I Halbfinale
Luuk de Jong wa Sevilla FC mfungaji wa bao la ushindi dhidi ya Man UPicha: Getty Images/I. Fassbender

Manchester United ya Uingereza  imefurushwa katika  awamu ya  nusu fainali  na  Seville  ya  Uhispania  baada  ya  kukubali kipigo cha  mabao 2-1 jana Jumapili. Kocha  wa Manchester United Ole Gunnar Solskjaer  amesema  kuwa anapanga  kuimarisha  kikosi  chake kabla ya  msimu  ujao  kuanza kufuatia  kipigo  hicho  ambacho  hakukitarajia  katika mchezo  wa nusu  fainali  mjini   Cologne jana  Jumapili.

Luuk de Jong akiweka kambani bao la ushindi kwa FC SevillaPicha: Getty Images/M. Meissner

Baada  ya  kuangukia  pua  mara  mbili  katika  awamu  ya  nusu fainali  katika  kuwania  vikombe msimu huu , United ilikuwa  inalenga kusongambele  hatua moja  zaidi  kwa  kufikia  fainali ya  Europa League Ijumaa  ijayo.

Walionekana mwanzoni  kuwa wanaelekea  kufanya  hivyo baada ya Bruno Fernandes  kuweka  mpira wavuni  kwa  penalti ikiwa ni penalti yao ya 22  ya  msimu  katika  dakika  ya  tisa ya  mchezo katika  uwanja wa  Rhine Energie  mjini  Cologne. Hata  hivyo , magoli kutoka kwa  winga wa Uhispania  Suso na mchezaji  wa zamani wa Newcastle United Luuk de Jong yalihakikisha  mabingwa mara tano wa Europa League  Seville watakumbana na  ama  Inter Milan ama Shaktar Donestsk  katika  fainali, wakati Man United ikimaliza  msimu bila  ya kupata taji.

Mfungaji wa bao la ushindi la  Seville Luuk de Jong  aliongoza kumwagia  sifa  mlinda mlango Yassine Bono  baada  ya  kufanya maajabu  kuokoa  mipira kadhaa  ya Manchester United katika mchezo  huo  wa  nusu  fainali  jana. Kocha wa  Seville Julien Lopetegui , ameisifu  kwa  jumla  timu  yake kwamba  ilicheza kwa moyo mkubwa.

Ni shangwe tupu kwa FC Sevilla wakishangilia ushindi dhidi ya Man United katika mchezo wa nusu fainali ya Europa LeaguePicha: Getty Images/M. Meissner

"Tulicheza kwa  moyo  mkubwa, wachezaji wajiamini, walikimbia. Tuliweza kucheza mpira katika kipindi cha  pili na kucheza vizuri zaidi,na kisha  goli lilipatikana. Tumefurahi  kupata nafasi katika fainali,  vijana  walifurahi sana, walistahili. Ni kikosi cha aina yake, wanastahili kucheza fainali. Tunafuraha kubwa kuwapa mashabiki wetu  kitu cha  kufuahia katika  wakati  huu  mgumu. Na sasa tuna ndoto ya  kucheza katika  fainali. Hatujui nani mpizani wetu , lakini bila  shaka  itakuwa ngumu  zaidi kuliko leo. Tunapaswa kujitayarisha."

Mchezaji aliyetokea katika benchi De Jong  aliwasha  moto kuwaingiza Seville  katika  fainali  ijayo  Ijumaa katika  dakika  ya  78, lakini  ni  pale Mmoroco Yassine Bono alipopambana  na mashambulizi  makali  ya  United peke  yake. Huyu  hapa Bono.

Mfungaji wa bao la Man United Bruno Fernandes akishangilia pamoja na Anthony Martial Picha: Getty Images/I. Fassbender

"Kama nilivyosema siku iliyopita, najihisi  wakati wote  kama sehemu ya  timu. Kila mara naweka mtazamo wangu  katika  malengo, nicheze au nisicheze , tushinde  ama  kushindwa. Kila mara najihisi kama nimo  ndani  ya  boti. Najaribu  kufanya kazi yangu, hakuna kingine, tunafahamu kuwa  mchezo ni wakati. Baadhi ya wakati unajitokeza na kufanya vizuri. Tulikuwa na  wakati  mgumu katika mchezo, lakini  tumethibitisha kuwa  ni timu  nzuri, tulikuwa na  mpira, tuliwafanya  waukimbize na  kuniruhusu mimi kupumua  kidogo."

Mlinda mlango wa FC Sevilla Mmorocco Yassine Bono akionesha ushujaa kwa kuzia mpira uliopigwa na Anthony Martial wa Man United (kushoto)Picha: Getty Images/M. Meissner

Ushujaa  aliouonyesha  Yassine Bono wa Seville, uliwaacha midomo wazi mashabiki  wa  kandanda  na  mashabiki  wa Manchester United wanahisi huyo ndie aliyewanyima hata kata ya maji.

Nilizungumza na mwenzangu katika  meza ya michezo DW idhaa  ya Kiswahili  Bruce Amani  kuhusu msisimko unaojitokeza  katika michezo  hii  ya  mtoano msimu  huu ya Champions League na Europa League, nae  alikuwa  na  haya  ya  kusema.

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW