1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SPD yawachagua Norbert Walter-Borjans na Saskia Esken

Sekione Kitojo
1 Desemba 2019

Wakosoaji wakubwa wa muungano unaounda serikali ya kihafidhina inayoongozwa na kansela  Angela Merkel  wameshinda uchaguzi katika uongozi wa chama cha Social Democrats SPD nchini Ujerumani siku ya Jumamosi (30.11.2019).

Deutschland Berlin SPD | Saskia Esken & Norbert Walter-Borjans, Sieger Mitgliederentscheid
Viongozi wapya wa SPD Walter-Borjans na Saskia Esken (kulia)Picha: Reuters/F. Bensch

Hali  hiyo  inazusha  maswali  mengi  kuhusiana  na  hatima ya serikali ya  Ujerumani. Chama  cha SPD  kimesema  mfuasi  wa siasa  za  mrengo  wa  kushoto Norbert Walter-Borjans na  Saskia Esken, ambao  waligombea  kwa  tikiti  ya  pamoja, walishinda asilimia 53.06 ya  kura  zilizopigwa  na  wanachama. Wanataka kujadili  upya  muungano  unaounda serikali  kulenga  zaidi  kuhusu haki  ya  kijamii, uwekezaji  na  sera za  mazingira.

Uongozi mpya wa chama cha SPD nchini UjerumaniPicha: Reuters/F. Bensch

Hata  hivyo , uwezekano wa  uchaguzi wa  haraka  ama  serikali yenye wingi  mdogo  bungeni umeongezeka  wakati wahafidhina wanaoongozwa  na  Merkel  huenda  wakakataa kutoa  ushirikiano licha  ya  kuwa  watapendelea  kubakia  mabadarakani.

Chama  cha  SPD , chama  kikongwe kabisa  nchini  Ujerumani, kimeingia  katika vurumai  baada  ya  kupata  matokeo  mabaya katika  chaguzi za  majimbo  na  uchaguzi  wa  bunge  la  Ulaya pamoja  na  mbio za  miezi  sita  kuwania  uongozi ambazo zimesababisha  chama  hicho kuporomoka  katika  maoni  ya  wapiga kura. Wanachama  wengi katika  uongozi  wa  chama  hicho wanona kuwa  kuokoka  kwao  ni  kujitoa  tu  kutoka  katika  serikali na kujenga  upinzani.

Pigo kwa Scholz

Wafuasi  hao  wawili  wa  siasa  za  mrengo wa  kushoto waliwashinda  waziri  wa  fedha  Olaf Scholz na  Klara Geywitz, ambao  walisema  watawaunga  mkono  mahasimu  wao  baada  ya ushindi wa  asilimia 45.33  ya  kura.

Christian Lindner, (kulia) wa chama cha FDP akizungumza wakati akiwa na kansela Angela Merkel (katikati) na Olaf Scholz (SPD) , (kushoto)Picha: picture-alliance/dpa/K. Nietfeld

Matokeo hayo  ni  pigo  kubwa  kwa  Scholz, mgombea  ambae ni maarufu  zaidi. Vyombo  vya  habari  vya  Funke  vimeripoti  kuwa hakusudii  kubakia  kuwa  waziri  wa  fedha.

Baada  ya  ushindi  wao  wa  kushitukiza, Walter-Borjans, waziri  wa fedha  wa  zamani  katika  jimbo  lenye  wakaazi  wengi  nchini Ujeruani  la  North Rhine-Westphalia  na  Esken, mbunge katika bunge  la  Ujerumani , Bundestag, wameahidi  kukileta chama  hicho pamoja  na  kujenga  umoja  miongoni  mwa  wanachama  na viongozi.

Walter-Borjans, ambaye  amepata  umaarufu  akifahamika  kama "Robin Hood" kwa  kupambana  na  wale  wanaokwepa  kulipa  kodi katika  benki za  Uswisi, amesisitiza  kuwa  chama  cha  SPD hakitautupilia  mbali  muungano  wa  serikali  mara  moja.

"Tumesema  mara  nyngi  hii  sio juu  ya  iwapo tunaondoka  mara moja  ama  kubakia  kwa kipindi fulani," aliiambia  televisheni  ya Phoenix, na  kuongeza  kuwa  analenga  kuangalia  sera  gani zinaweza  kutekelezwa pamoja  na  chama  cha  Merkel na  zipi haziwezekani.

Mwenyekiti mpya wa SPD Norbert Walter-Borjans akizungumza baada ya kuchaguliwa kukiongoza chama cha SPDPicha: Reuters/F. Bensch

Viongozi  hao  wawili  wamesisitiza kwamba  wanataka  wahafidhina kukubaliana  na  kiwango  cha  juu  cha   mshahara  wa  kima  cha chini  na  uwekezaji  zaidi  katika  miundo  mbinu pamoja  na  ulinzi wa  mazingira, iwapo  itahitajika hata  kwa  kuwa  na  deni  jipya.

Katibu  mkuu wa  chama  cha  Christian Democrats CDU  amesema chama  chake  kinataka  kufanyakazi  pamoja  na  uongozi  mpya  wa SPD na  kwamba  vyama  hivyo  tayari  vina  msingi  wa  pamoja  wa kufanyia  kazi.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW