Starmer asema Ulaya imeungana kwaajili ya Ukraine
10 Desemba 2025
Ametoa kauli hiyo baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kusema bara hilo linaporomoka.
Katika mahojiano aliyofanyiwa na jarida la Politico la Marekani, Trump aliwaita viongozi wa Ulaya kuwa dhaifu na kuikosoa Ulaya kushindwa kumaliza vita vya Ukraine.
Haya yanatokea wakati Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky akisema yuko tayari kuitisha uchaguzi ndani ya siku 60 hadi 90, hata wakati nchi yake ikiwa vitani, iwapo Mrekani na Ulaya zitamuhakikishia usalama.
Zelensky ameongeza kuwa kufanya hivyo, kutahitaji mabadiliko ya sheria ya uchaguzi.
"Ninaomba manaibu wa kundi letu, hasa wabunge wetu, waandae mapendekezo kuhusu uwezekano wa kuifanyia mabadiliko sheria za uchaguzi chini ya sheria ya kijeshi. Nitayarishieni haya. Nitakuwa Ukraine kesho na ninatarajia kupata mapendekezo kutoka kwa washirika wetu, ninatarajia kuona mapendekezo kutoka kwa manaibu wetu, na niko tayari kuendelea na uchaguzi."
Rais huyo wa Ukraine ametoa kauli hiyo baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kumshutumu kwa kung'ang'ania madarakani.