1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sudan Kusini yaanza mchakato wa kuandika rasimu ya katiba

26 Mei 2021

Sudan Kusini imeanza kuandika rasimu ya mwisho ya katiba kwa lengo la kuuongeza nguvu mpango tete wa amani ikiwa ni mwongo mmoja baada ya nchi hiyo kupata uhuru.

Südsudan Salva Kiir und Riek Machar | Entscheidigung für  Einheitsregierung
Picha: AFP/A. McBride

Rais Salva Kiir aliongoza sherehe ambayo iliuzindua mchakato huo, kama sehemu ya mpango wa amani uliofikiwa na mpinzani wake. Riek Machar mwaka wa 2018.

Nchi hiyo changa kabisa duniani, imekuwa ikiongozwa na katiba za muda wakati wa miaka iliyogubikwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyofuatia uhuru wa nchi hiyo Julai 2011.

soma zaidi: Migawanyiko ya kisiasa Sudan Kusini imezidisha uhasama

Akizungumza baada ya uzinduzi huo jana, Rais Kiir alisema warsha hiyo inalenga kutengeneza mpango wa kupatikana katiba ya kudumu ya Jamhuri ya Sudan Kusini.

Alisema ni muhimu sana ionyeshe matakwa ya watu ya uhuru, usawa, haki na ustawi kwa wote. Hafla hiyo ilihudhuriwa na pande zote zilizosaini muafaka wa 2018, pamoja na wajumbe wa kimataifa kutoka Umoja wa Afrika, Umoja wa Ulaya na Umoja wa Mataifa.