1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

Sudan: Siku ya tatu ya mapigano yapelekea vifo vya watu 97

17 Aprili 2023

Mji mkuu wa Sudan, Khartoum, unakabiliwa na siku ya tatu ya mapigano makali kati ya makundi pinzani ya jeshi, ambayo hadi sasa yamesababisha takribani watu 100 kuuawa.

Kämpfe im Sudan
Picha: Marwan Ali/AP/dpa/picture alliance

Mashambulizi ya anga na makombora yameendelea kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali ya mji mkuu Khartoum na mji jirani wa Omdurman. Milio ya risasi na mabomu vilisikika pia karibu makao makuu ya jeshi, huku moshi mweupe ukionekana kutoka eneo hilo.

Wakaazi wa jiji la Khartoum wamesalia majumbani mwao huku wakiripoti pia kukatika kwa umeme na matukio kadhaa ya uporaji.

Mapigano hayo ni sehemu ya mzozo wa kugombea madaraka  kati ya kamanda wa jeshi Jenerali Abdel-Fattah al-Burhan, na Jenerali Mohammed Hamdan Dagalo, mkuu wa kikundi cha kijeshi cha Rapid Support Forces (RSF).

Soma pia: Umoja wa Afrika wakutana kuijadili Sudan 

Majenerali hao wawili ni washirika wa zamani ambao walipanga kwa pamoja mapinduzi ya kijeshi ya Oktoba mwaka 2021 ambayo yaliharibu mchakato wa mpito na wa muda mfupi wa Sudan kuelekea kwenye demokrasia.

Jenerali Abdel-Fattah al-BurhanPicha: Marwan Ali/AP/dpa/picture alliance

Wawili hao wamekaidi na kusema hawatofikia makubaliano ya kusitisha mapigano, huku kila upande ukimtaka mwengine kujisalimisha. Hata hivyo pande zote mbili zina wafadhili wa kigeni wenye nguvu, jambo linaloweza kupelekea uwezekano mkubwa wa kusababisha shinikizo la kidiplomasia.

Jenerali Mohammed Hamdan Dagalo, mkuu wa kikundi cha kijeshi cha Rapid Support Forces (RSF).Picha: Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance

Tangu mapigano yalipozuka siku ya Jumamosi, raia wapatao 97 wameuawa na mamia ya wengine wamejeruhiwa, hayo ni kwa mujibu wa Shirika la Madaktari la Sudan, linalounga mkono vuguvugu la kidemokrasia na kufuatilia hali ya majeruhi. Hata hivyo, hakujakuwa na taarifa rasmi kuhusu idadi ya wapiganaji waliouawa.

Soma pia:  Karibu watu 56 wauawa katika machafuko nchini Sudan

Moshi ukionekana kufuatia mapigano kati ya pande mbili pinzani za Jeshi nchini Sudan (16.04.2023)Picha: Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance / AA

Matukio ya machafuko yaliyogubika mizinga, silaha mbalimbali na ndege za kivita katika maeneo yenye watu wengi katika mji mkuu wa Sudan, ni hali ya kutisha ambayo haijawahi kushuhudiwa huko Khartoum. Sudan ina historia ndefu ya mapigano ya wenyewe kwa wenyewe, lakini mapigano mengi yamekuwa yakifanyika katika maeneo ya kikabila na yaliyo mbali na mji wa Khartoum.

Hofu ya Jumuiya ya kimataifa

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony BlinkenPicha: Andrew Harnik/AP/picture alliance

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken amesema:

"Kuna wasiwasi mkubwa kwa sote kuhusu mapigano na ghasia zinazoendelea nchini Sudan. Tishio ambalo linawakabili raia na ambalo linalikabili taifa la Sudan. Tishio hilo linaweza kusambaa katika eneo zima."

Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Volker Perthes ametaja kusikitishwa na hatua ya vikosi pinzani vya kijeshi kutoheshimu kikamilifu usitishaji mapigano wa muda uliokubaliwa na pande zote hapo jana ili kuwahamisha majeruhi.

Jumuiya ya kimataifa imezitaka pande zote mbili kusitisha mapigano   yaliyozuka wakati waislamu nchini humo na duniani kote wakiwa katika siku za mwisho za mafungo ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW