1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watetezi karibu 200 wa mazingira waliuawa 2023

Sylvia Mwehozi
11 Septemba 2024

Ripoti ya kila mwaka ya Shirika la kimataifa la Global Witness, imeeleza kuwa takribani wanaharakati 200 wa mazingira duniani kote waliuawa mwaka jana, 2023.

Bango lenye ujumbe kulinda sayari
Bango lenye ujumbe kulinda sayariPicha: TOBIAS SCHWARZ/AFP/Getty Images

Ripoti hiyo pia imemulika ukandamizaji dhidi ya wanaharakati wa mazingira nchini Uingereza, Ulaya na Marekani. Kanda ya Amerika Kusini inasalia kuwa eneo hatari duniani kwa wapigania haki wa mazingira, ikiwa na karibu asilimia 85 ya mauaji 196 yaliyorekodiwa mwaka jana.Nchi tajiri zalaumiwa kwa kitisho cha kimazingira

Colombia, Brazil, Honduras na Mexico ndio nchi zinaongoza katika ripoti hiyo. Shirika hilo liliorodhesha vifo 79 nchini Colombia pekee.

Ripoti hiyo pia iliangazia idadi ya watu waliokufa nchini Honduras, ambayo ilirekodi mauaji 18, idadi kubwa zaidi. Miongoni mwao alikuwa ni baba aliyeuawa pamoja na mtoto wake mwenye umri wa miaka 15.

Barani Afrika, kumerekodiwa vifo vinne pekee lakini kuna wasiwasi kuwa huenda takwimu hizo ni makadirio ya chini kutokana na changamoto ya kukusanya taarifa.

Maandamano ya mabadiliko ya tabia nchi BerlinPicha: TOBIAS SCHWARZ/AFP/Getty Images

Mwandishi wa ripoti hiyo Laura Furones alisema kuwa "kadri mzozo wa mabadiliko ya tabia nchi unavyoongezeka, wale wanaotumia sauti zao kwa ujasiri kutetea sayari yetu wanakabiliwa na ukatili, vitisho na mauaji". Ameongeza kuwa "data zetu zinaonyesha kwamba kiwango cha mauaji kinasalia kuwa cha kutisha, hali ambayo haikubaliki".

Soma: Wanaharakati wanaopinga mradi wa mafuta Uganda wakamatwa

Kulingana na ripoti hiyo, wanaharakati wanaofanya kampeni dhidi ya uchimbaji madini, uvuvi, ukataji miti, kilimo biashara, barabara na ujenzi wa miundombinu na mitambo ya kuzalisha umeme wanaishi kwa hatari. Uhalifu mwingi unapita bila kuadhibiwa.

Kwa mujibu wa Furones, serikali hazipaswi kufumbia macho; ni lazima zikchukue hatua za kuwalinda watetezi na kushughulikia sababu zinazochangia ukatili huo.Mwanaharakati wa mazingira ahukumiwa miezi 16 Ujerumani

"Wanaharakati na jumuiya zao ni muhimu katika jitihada za kuzuia na kurekebisha madhara yanayosababishwa na viwanda vinavyoharibu hali ya hewa. Hatuwezi kumudu, wala hatupaswi kuvumilia, kupoteza maisha tena."

Huko Asia, Ufilipino imeendelea kuwa mahali hatari zaidi kwa ulinzi wa mazingira na ardhi, na mauaji 17. Ripoti ya Global Witness ilionyesha mwelekeo unaoongezeka wa utekaji nyara katika kanda hiyo.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW