1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Taliban yaiandikia Marekani barua ya wazi

17 Novemba 2021

Katika barua ya wazi kwa bunge la Marekani, watawala wa Taliban nchini Afhganistan wanaihimiza Marekani kushughulikia mgogoro wa kibinadamu na kiuchumi unaofukuta nchini humo

Afghanistan Still Lebensmittelhilfe
Picha: AFP

Barua hiyo iliyotiwa saini na waziri wa mambo ya nje wa uongozi wa Taliban Amir Khan Mutaqi na kutolewa Jumatano (17.11.2021)  inatoa wito kwa Marekani kuachilia mali ya benki kuu ya Afghanistan huku ikiongeza kuwa changamoto kuu ilioko kwa sasa kwa watu wa taifa hilo ni uhaba wa fedha, hali inayotokana na kuzuiliwa kwa mali ya watu wa taifa hilo na serikali ya Marekani. Barua hiyo imeendelea kusema kuwa uongozi wa Taliban una wasiwasi kwamba iwapo hali iliyoko kwasasa itaendelea, itasababisha uhamaji mkubwa wa watu na kuharibu sekta za afya na elimu nchini humo.

Barua hiyo pia imesema kuwa mateso ya watoto kutokana na utapimlo , kifo cha mama kutokana na ukosefu wa huduma bora za afya, kunyimwa chakula, makazi, dawa na mahitaji mengine ya kimsingi kwa raia wa kawaida wa taifa hilo hakuna uhalalishaji wa kisiasa ama wa kimantiki na ni hatari kwa ufahari wa serikali na watu wa Marekani kwasababu ni dhahiri kwamba ni suala la kibinadamu.

Rais wa Marekani - Joe BidenPicha: Susan Walsh/AP/picture alliance

Wakati kundi la Taliban lilipochukuwa mamlaka kwa nguvu nchini Afghanistan mnamo mwezi Agosti, misaada mingi kwa taifa hilo ilisimamishwa. Takriban bilioni 9 katika akiba ya benki kuu nchini humo nyingi zikiwa zimewekezwa nchini Marekani, zilizuiwa. Kabla ya hapo, serikali ya Afghanistan ilikuwa imepokea dola bilioni 8.5 kwa msaada wa kijeshi na kiraia wa kila mwaka kulingana na ripoti ya mtandao wa wachambuzi wa Afghanistan ulioko mjini Kabul. Misaada hiyo ilitumika kufadhili asilimia 75 ya matumizi ya umma.

Kufikia sasa, mamilioni ya watu wamepoteza chanzo chao kikuu cha mapato huku sekta za afya pamoja na huduma nyingine za umma zikikosa kufanya tena kazi kikamilifu. Mashirika ya misaada wa kibinadamu yameonya kuwa mmoja kati ya wanawake wanne na mmoja kati ya watoto wawili wana utapiamlo. Mashirika hayo yanayotoa huduma zao nchini Afghanistan yanasema kuwa nusu ya idadi ya watu nchini humo hawajui mlo wao unaofuata utatoka wapi. Umoja wa Mataifa umeonya kuwa asilimia 97 ya Waafghanistan huenda wakatumbukia katika umaskini kufikia katikati ya mwaka 2022.