1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TANZANIA IMEJITOA KATIKA CHANGAMOTO ZA KOMBE LA AFRIKA MASHARIKI NA KATI NCHINI SUDAN

1 Desemba 2003
-ENYIMBA YA NIGERIA YAILAZA ISMAILIA YA MISRI 2:0 KATIKA DURU YA KWANZA YA FINALI YA KOMBE LA KLABU BINGWA BARANI AFRIKA
-NA KURA IMEPIGWA KWA KOMBE LA ULYA LA MATAIFA NCHINI URENO MWAKANI

VFB Stuttgart ya ujerumani, Chelsea ya Uingereza na AC Milan ya Itali zilisherehekea ushindi wao wa kati ya wiki katika champions League-kombe la klabu bingwa barani Ulaya kwa kuparamia kileleni mwa Ligi za nyumbani mwishoni mwa wiki.mabingwa wa Ujerumani -Bayern munich nusra wakione kilichomtoa kanga manyoya katika mpambano wao na FC Cologne inayoburura mkia wa Ligi.

Borussia Dortmund waliopigwa kumbo nje ya Kombe la ulaya la UEFA kati ya wiki walipata jana pigo jengine la kuzabwa mabao 2-1 na Hansa Rostock.
Stuttgart imepanua mwanya wa pointi 2 kileleni na kurefusha rekodi yao ya kutoshindwa msimu huu hadi mapambano 14.Hatahivyo, jumamosi Stuttgart ilimudu suluhu tu 0:0 kati yake na Bochum.
Hamburg pia ilizimwa bao 1:1 na Bremen inayosimama nafasi ya pili ya ngazi ya Ligi.Halkadhalika bayer Leverkusen ilitoka suluhu 2:2 na Munich 1860.
Kiroja cha mambo kiliifika bayern Munich-mabingwa wa Ujerumani.Munich ikicheza nyumbani na FC Cologne ambayo ni ya mwisho katika orodha ya ligi ilikaribia kushindwa na mwishoe ilivuka salama tu 2:2 .Cologne ilitangulia kwa kutia bao pale msham,bulizi wao Andre Voronic alimponasa wavu wa oliver kahn wakiwa uso kwa uso.hii ilikua dakika ya 35 ya mchezo.Munich ilisawazisha na kuongoza kwa mabao 2 ya Claudio Pizzaro wa Peru.Lakini Cologne,licha ya kuburura mkia wa Ligi haikujificha ilisawazisha na laiti ingelikua na bahati ingeondoka na ushindi kwani ilikosea kidogo tu kutia bao katika dakika ya mwisho ya mchezo.

Stuttgart inaongoza orodha ya Ligi kwa pointi 34 ikifuatwa na Bremen yenye pointi 32.Leverkusen iko nafasi ya 3 kwa pointi 31 na mabingwa Munich wameangukia nafasi ya 4 kwa pointi 28.
Mkiani mwa Ligi bado zipo FC Cogologne,Frankfurt na Hertha Berlin ambayo kocha wake Jupp Stevens hatima yake haijulikani.

KURA YA KOMBE LA ULAYA LA MATIAIFA 2004 IMEPIGWA JANA MJINI LISBON,URENO:
Finali ya Kombe hilo itachezwa katika viwanja 10 mbali mbali kati ya Juni 12 na Julai 4 mwakani.
Mahasimu wa kale Ujerumani na Holland kwa muujibu wa kura ya jana watakutana katika kundi gumu kabisa kati ya yote-kundi D:

Ni kundi linalojumuisha pia Jamhuri ya czech na chipukizi pekee Latvia.
Kura ya Kombe hilo la Ulaya nchini Ureno,Juni mwakani, imekumbanisha pia timu nyengine kali kama vile wenyeji Ureno wakipangwa kucheza na jirani spain na mabingwa wa Ulaya Ufaransa wakikutanishwa na Uingereza katika mechi zao za kwanza.
Ureno pia inakutana na russia na Ugiriki katika kundi A.Ufaransa inapaswa kucheza na jirani mwengine mbali na Uingereza nae ni uswisi pamoja na Croatia katika Kundi B.

Katika kundi C ,Itali,Sweden,Danmark na Bulgaria zinakutana.
Ujerumani na Holland zote mbili zimeungama kuwa wao utakua mpambano mgumu na wa kukata na shoka na utafufua uhasama wao wa dimba. Majirani hao 2 watakutana katika changamoto yao ya kwanza ya Kombe hilo hapo juni 15 na mpambano huo utaamua hatima ya kila mmoja katika kombe hilo la Ulaya.
Kocha wa ujerumani Rudi Völler binafsi alihusika na kisa kimoja cha mvutano kati ya wachezaji wa pande hizi mbili:Hii ilikua katika Kombe la dunia 1990 nchini Itali pale Völler alipotimuliwa nje ya uwanja na rifu kwa kumtemea mate Frank Rijkaard wa holland ambae pia alionywa kwa kadi nyekundu.

FINALI YA I YA KOMBE LA KLABU BINGWA AFRIKA:
Duru ya kwanza ya finali ya klabu bingwa imemalizika jana kwa ushindi wa mabao 2:0 wa Enyimba ya Nigeria dhidi ya Ismailia ya Misri mjini Aba,Nigeria.
Mabingwa hao wa Nigeria wangeliweza hata kushinda kwa wingi mkubwa zaidi wa magoli ili kumaliza udhia na mapema laiti hawangepoteza nafasi kadhaa za kutia mabao pamoja na kuokoa maridadi kwa kipa wa Misri Mohammed Sobhi.
Emeka Nwanna alifungua mlango kwa bao la kwanza la Enyimba katika dakika ya 28 ya mchezo.Anumnu akaipatia Enyimba bao la pili .

Enyimba inatapia kuwa klabu ya kwanza ya Nigeria kuvaa taji la kombe la klabu bingwa barani Afrika tangu kupita miaka 35.Pengine, jana Enyimba imepoteza nafasi nzuri ya kuhakikisha Kombe hilo kweli linakuja Nigeria.Kwani katika duru ya pili na ya mwisho ya finali hii nyumbani mwa Ismailia,mizinga yote ya wamisri itaelekezwa Nigeria.

KOMBE LA AFRIKA MASHARIKI NA KATI-CHALLENGE CUP NCHINI SUDAN:
Kombe hilo likiendelea,Tanzania-mojawapo ya nchi waasisi wa kombe hili kuanzia enzi ya Gossage Cup,imejitoa kutoka changamoto za mwaka huu huko Sudan.
Tanzania yadai kwamba imejitoa kutoka mashindanoni baada ya kushindwa kujipatia usafiri wa ndege kutoka Nairobi hadi Khartoum-amesema Yahya Mhata, mwenyekiti wa Tume ya mpito ya FAT-chama cha mpira cha Tanzania-bara.Alieleza kwamba ndege iliokua ipakie timu ya Tanzania ilijaa kabisa.

Tanzania yaweza sasa kupigwa faini ya hadi dala 20.000.Taifa Stars kama chama cha mpira cha Tanzania-FAT imeo katika msukosuko mkubwa na sio tu kwa kujitoa kwa Tanzania katika Kombe la Challenge Cup huko Sudan: FAT imegawika na mjumbe wa FIFA alibidi kwenda tanzania kusaka ufumbuzi na kumaliza mvutano.Bado halikupatikana suluhisho.

Kombe la Dunia la vijana limeanza huko Dubai,uarabuni:
Rais wa FIFA Sepp Blatter amezisham,bulia zile klabu zilizokataa kuwatoa wachezaji wao kwa ajili ya Kombe hili la timu za chini ya umri wa miaka 20. Hasa Boca Juniors ya Argentina imeamua kutowatoa wachezaji wake muhimu.Bocca imepangwa kucheza na mabingwa wa Ulaya AC Milan hapo desemba 14 katika kinyan'ganyiro cha Kombe lisilo rasmi la klabu bingwa ya dunia.
Hapo jumamosi, Ivory Coast mojawapo ya waakilishi wa Afrika katika Kombe hili iliilaza Mexico kwa mabao 2:1 na Misri ikamudu sare 0:0 na Colombia. Ujerumani ilichapwa mabao 2:0 na Korea ya kusini.
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW