1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania kuendeleza sekta ya nishati

14 Februari 2023

Serikali ya Tanzania leo imetia saini mikataba 26 ya uzalishaji umeme utakaopelekwa katika maeneo maalumu yakiwemo ya wajasiliamali wadogowado na wakulima, huku ikisisitiza kuendeleza nishati hiyo.

Tansania Präsidentin Samia Suluhu Hassan startet Wasserprojekt in Dar es Salaam
Picha: President of Tanzania Office

Katika hafla ambayo imeshuhudiwa na Rais Samia Suluhu Hassan imefanyika ikulu jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali, wakiwamo washirika wa kimaendeleo kutoka nchi za Magharibi.

Hiyo ikitajwa ni hatua inayolenga kuondokana na adha ya ukosefu wa umeme wa uhakika inayojitokeza mara kwa mara katika maeneo mengi ya nchi.

Hatua hii inatazamwa kama dawa itayokwenda kutibu tatizo hilo linaloonekana kuota mizizi wa miaka mingi.

Mikataba 26 iliyosainiwa kwa wakati mmoja, itagusa maeneo kama vituo vya afya, wachimbaji wadogo wadogo, wakulima pamoja na usambazaji wa huduma hiyo katika maeneo ya vijijini.

Soma pia:Rais Samia akosowa mfumo wa utoaji haki

Akizungumza baada ya zoezi la kutia saini kati ya serikali na makampuni ya kikandarasi Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan,amesema jukumu la kiongozi ni kutetea maslahi ya kimsingi kwa wananchi.

Amesisitiza kuwa kiu ya serikali yake ni kuwafikishia wananchi huduma muhimu na  kile kilichofanywa leo ni hatua ya kuwafanya wananchi wawe sehemu ya maendeleo ya nchi na kuwapunguzia adha wanazokumbana nazo.

Kipaumbele katika nishati Tanzania

Kila mwaka serikali imesema itatenga kiasi cha bilioni 500 kwa ajili ya kuendeleza miradi ya usambazaji umeme.

Ikiwemo pia kuifanyia ukarabati mitambo iliyopo kwamba kazi hiyo itafanywa kwa awamu kadhaa hadi pale maeneo yote ya nchi yatakapokuwa yamefikiwa kikamilifu na huduma hiyo ya nishati ya umeme.

Kukamilika kwa miradi hiyo kwa kiasi kikubwa itakuwa ni habari njema kwa wakazi wengi wanalalamika juu ya uhaba wa nishati hiyo.

Waziri wa nishati, January Makamba amesema mbali ya miradi hii, kadhalika wizara yake inakusudia kutupia macho vyanzo vingine vya uzalishaji umeme kama vile umeme utokanao na nishati jadidifu ikiwemo upepo.

Soma pia:Tanzania, Kenya zapiga hatua katika kupambana na rushwa-CPI

Amedokoza pia kuhusu umeme utakazalishwa kutoka bwawa la Julius Nyerere liloko katika hifadhi ya Selou akisema kazi ya kuzaja maji inaendelea vyema.

Bwawa hilo ambalo ujenzi wake ulimilika katika miezi ya hivi karibuni, huenda likaanza kuzalisha umeme wa majaribio mapema mwakani.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW