1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania: Polisi anayehusishwa na ubakaji afikishwa kortini

Deo Kaji Makomba
5 Septemba 2024

Afisa wa polisi anayetuhumiwa kulituma na kulifadhili genge la vijana kumbaka na kumlawiti msichana mmoja, amefikishwa mahakamani kwenye mji mkuu wa Tanzania Dodoma kujibu tuhuma zinazomkabili.

Tanzania I Mshukiwa wa kadhia ya ubakaji afikishwa mahakamani Dodoma
Polisi anayeshukiwa kupanga sakata la ubakaji nchini Tanzania afikishwa mahakamani Dodoma.Picha: Deo Kaji Makomba/DW

Afisa huyo Fatma Kigondo anadaiwa kuwa ndiye "Afande" aliyekuwa akitajwa na kundi hilo la vijana lilipokuwa likimfanyia vitendo vya kikatili  msichana huyo aliyepachikwa jina la "Binti wa Yombo". 

Awali shauri hilo linalomuhusisha Fatma Kigondo ambaye ni afisa wa jeshi la polisi nchini Tanzania lilipangwa kwa mara ya kwanza Agosti 23 mwaka huu mbele ya hakimu mkazi wa mahakama ya mkoa wa Dodoma Francis Kishenyi, na siku hiyo afande Fatma Kigondo hakufika mahakamani na shauri hilo kuahirishwa hadi leo Septemba tano.

Mtuhumiwa afande Fatma Kigondo alifika mahakamani leo hii huku akiwa amejifunika gubigubi na hivyo kuwa vigumu kwa wandishi wa habari kutambua aliingia muda gani mahakamani hapo. Hata hivyo shauri hilo limeahirishwa tena hadi Oktoba saba mwaka huu kufuatia hakimu Francis Kisenyi aliyekuwa na kesi hiyo kuhamishwa kituo cha kazi.

Wito watolewa kutokomezwa kwa dhuluma zote za kingono Tanzania.Picha: Colourbox

Soma pia: Tanzania, Kamanda ahamishwa baada ya kauli iliyozusha hasira

Paul Kisabo ni wakili aliyefungua kesi hiyo anasema:

"Tumepewa taarifa kwamba, hakimu Francis Kisenyi amehamishwa kituo cha kazi kwahiyo shauri lilipangwa kuhairishwa mbele ya muheshimiwa tungalaja nay eye mamlaka yake katika shauri hili ilikuwa ni kuahirisha tu kwasababu shauri hili halijapangiwa bado hakimu wa kulisikiliza, lakini siku ya leo pia Fatma Kigondo alifika mahakamani na hivyo shauri limeahirishwa hadi tarehe saba mwezi wa kumi mwaka 2024 katika mahakama hii ya hakimu mkazi Dodoma. Tunaamini siku hiyo tutakuta shauri limepangiwa hakimu kwa ajili ya kusikiliza na kama itakuwa imeishapangiwa tayari, maana yake usikilizaji wa kesi hii utaanza mara moja.”

Hatua hiyo ya hakimu wa shauri hilo la Afande anayetuhumiwa kufadhili tukio la ubakaji na ulawiti kwa binti wa Yombo Dovya Jijini Dar es Salaam kupangiwa kituo kingine cha kazi imeibua hasira na maoni mseto kutoka kwa makundi mbalimbali wakiwemo wanaharakati wa kutetea haki za binadamu. Charles Odero anatoka katika asasi yaUraia na msaada wa kisheria, iliyoko Arusha kaskazini mwa Tanzania amesema "Sasa kama kweli mahakama ilijua kwamba kesi hii ina umuhimu wake, lakini cha ajabu kwamba mahakama hiyo hiyo inaweza ikamuhamisha hakimu na bila kuweza kumpangia hakimu mwingine  majukumu haya ya kusikiliza hiyo kesi kwa hiyo sisi kwetu kwakeli inasikitisha na kwetu sisi ni kwamba mahakama ya Tanzania inazidi kujiondolea uhalali wake kwa wananchi. Uhalali wake utabaki kwenye makaratasi ya sheria kwahiyo wananchi wataidharau mahakama.”

Tanzania: Vitendo vya kikatili dhidi ya wanawake vikomeshwe

02:52

This browser does not support the video element.

Tayari washitakiwa wanne wamefunguliwa kesi ya ubakaji kwa kundi na kuingilia kinyume na maumbile binti huyo wa Yombo Dovya jijini Dar es salaam kesi ambayo iko mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Dodoma mbele ya hakimu mkuu mkazi, Zabibu Mpangule.

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW