Tanzania: Serikali inaendelea na juhudi za kulinda amani
16 Februari 2026
Akizungumza katika mkutano na vyombo vya Habari kuhusu ziara za kikazi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Waziri wa mambo ya nje, Mohamed Thabit Kombo amesema Rais Samia amezungumzia changamoto ya vurugu za Oktoba 29 wakati wa uchaguzi mkuu wa Tanzania zilizoikumba Tanzania na jitihada zinazofanywa na nchi.
“Daktari Samia Suluhu Hassan pia alielezea changamoto zilizotokea nchini kwake na kueleza jitihada zilizofanyika bila kuhitaji msaada kutoka nje, sisi tunaweza kuwa na changamoto kubwaa lakini za kwetu zinaweza kuwa kama punje tu ya ngano”
Kadhalika Waziri Kombo amesema, Rais aliwasilisha mbele ya marais wenzake jitihada za serikali yake za kuendelea kulinda amani ya Tanzania, ikiwamo kuundwa kwa tume huru ya uchunguzi wa vurugu hizo sambamba na kuundwa kwa wizara ya vijana na wizara mpya ya mahusiano ya jamii huku akisisitiza kuwa, vurugu za Tanzania ni ndogo ukilinganisha na za nchi nyingine za Afrika.
Ziara ya Addis Ababa yammpa Samia Mafanikio makubwa
Katika hafla hiyo ya Ikulu, wanahabari walielezwa mafanikio makubwa aliyoyapata Rais katika ziara hiyo ikiwamo Rais Samia katika sekta ya maji sambamba na kutunukiwa tuzo ya rais wa kimataifa wa ubunifu katika sekta ya maji kwa mwaka 2025 kutoka taasisi ya Maji ya Kimataifa(Global water Partnership) kadhalika alitunukiwa tuzo ya kinara wa maji na usafi wa mazingira na usafi binafsi, kutoka taasisi ya Water Aid ya Uingereza. Naibu Waziri Wa Maji, Mhandisi Mathew Kundo ameeleza.
“Alitunukiwa tuzo ya rais wa kimataifa ya ubunifu katika sekta ya maji, heshima kubwa iliyotoelwa kutoka taasisi ya maji, Th Global water partnership. Lakini pamoja na mafanikio hayo pia, Mheshimiwa rais alitunukiwa tuzo ya kinara wa maji na usafi wa mazingira na usafi binafsi”
Mkutano wa Umoja wa Afrika kwa mwaka huu ulibebwa na kauli mbiu isemayo; “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Mifumo Salama ya Usafi wa Mazingira ili Kutimiza Malengo ya Agenda 2063. Moja ya matukio muhimu ya mkutano huo ilikuwa ni kukabidhiwa rasmi uenyekiti wa Umoja wa Afrika kwa Rais wa Burundi, Évariste Ndayishimiye, akimrithi Rais wa Angola, João Lourenço.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Gutteres amesema:
"Huu ni mwaka 2026 na sio 1946 na chochote kitakachojadiliwa kuhusu Afrika, Afrika lazima iwepo mezani”
Kadhalika wanahabari walielezwa masuala makuu yaliyojadiliwa katika mkutano huo wa AU ikiwamo Amani na Usalama barani Afrika, ugaidi na migogoro inayoendelea katika baadhi ya nchi za Afrika.
Mengine ni masuala ya Afya na Uhuru wa Dawa Barani Afrika ambapo Mkutano huo ulihitimishwa kwa kupitishwa kwa maazimio na maamuzi muhimu yanayothibitisha dhamira ya Afrika kutekeleza kwa vitendo dira ya Agenda 2063 — “Afrika Tunayoitaka.”