1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania yatangaza mkakati wa kuwalinda watu wenye ualbino

George Njogopa20 Juni 2024

Serikali ya Tanzania imeelezea msimamo wake kuhusu hatima ya watu wenye ualbino, ambapo imeandaa mikakati maalumu ya kuwalinda watu wenye ualbino inayoanza kutekelezwa mara moja.

Mapambano dhidi ya ualbino
Vitendo vya kuwaandama watu wenye ualbino vilishika kasi miaka kumi iliyopitaPicha: TONY KARUMBA/AFP/Getty Images

Tamko hilo limetolewa kufuatia mauaji ya hivi karibuni ya mtoto mwenye ualbino Asimwe Novart ambaye mwili wake uliokotwa mkoani Kagera huku baadhi ya viungo vyake vikiwa vimenyofolewa. Hayo yanajiri wakati ambapo jeshi la polisi nchini humo likitangaza kuwa limewakamata watu tisa wanaotuhumiwa kwa mauji ya mtoto huyo. 

Akizungumza bungeni mjini Dodoma, Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema hatua ya kuwalinda watu wenye ualbino ni jambo linalopaswa kutelelezwa na makundi yote ya jamii na kwa upande wake serikali imeweka hatua kadhaa ambazo utekelezaji wake utahusisha wakuu wa mikoa, wilaya, vyombo vya dola, viongozi wa dini pamoja na watoa tiba za jadi.

Rais Samia Suluhu Hassan amekemea kisa cha kuuawa mtoto wa mwenye ualbino Picha: Presidential Press Service Tanzania

Katika utekelezaji huo, Julai 3 wakuu wa mikoa pamoja na wasaidizi wao watakutana kwenye kikao cha pamoja kitachokuwa na jukumu la kuratibu na kuanisha mikakati ambayo itatoa majibu ya namna ya kuanzisha ulinzi mahsusi kwa ajili ya watu wenye ualbino.

Waziri huyo mkuu amesema kama hatua nyingine ya kuwahakikishia usalama, watu wenye ualbino watasajiliwa nchini kote kwa ajili ya kuanzisha kanzi data itakayosaidia kujua changamoto zinazowakabili na hatimaye kuzitolea majawabu mara moja.

Ama amewaonya waganga wa jadi wanaojitumbukiza katika vitendo vya kishirikina ikiwamo kuhamasisha ramli chonganishi kuacha mara moja akisema watu wenye ualbino ni binadamu kama iliovyo wengine wa kawaida.

Soma pia: Utetezi wa albino nchini Tanzania

Hatua hiyo ya serikali inachukuliwa siku moja baada ya jeshi la polisi kutangaza kuwatia mbaroni watu tisa akiwamo baba mzazi wa mtoto aliyeuawawa na msaidizi wa paroko wanaotuhumiwa kuhusika katika mauiji ya mtoto Asimwe Novart ambaye mwili wake uliokotwa majuzi huku baadhi ya viungo vyake vikiwa vimenyofolewa.

Unyanyapaa dhidi ya walemavu wa ngozi ungalipo

01:21

This browser does not support the video element.

Msemaji wa jeshi la polisi, David Misiime katika taarifa yake alisema kutiwa mbaroni kwa watuhumiwa hao kulifuatiwa na operesheni kali iliyoendeshwa wilayani Muleba, mkoani Kagera.

Mtoto Asimwe alichukuliwa nyumbani kwao kaskazini magharibi mwa Tanzania katika kijiji cha Bulamula, wilayani Muleba, Kagera Mei 30 majira ya saa mbili usiku.

Vitendo vya kuwaandama watu wenye ualbino vilishika kasi miaka kumi iliyopita katika maeneo ya mikoa ya Kanda ya Ziwa kabla ya opereshini kali ya kuwasaka wahusika wake hatua iliyosaidia kumalizika kwa matukio hayo.

Hata hivyo, kuzuka tena kwa vitendo hivyo kumeisukuma serikali kutangaza mikakati mipya ambayo utekelezaji wake unaanzia ngazi ya taifa mpaka mashinani.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW