Iran yaapa kujibu vitisho vya Trump, Hormuz
22 Machi 2026
Marekani na Iran zinatishia kuvizidisha vita vyao, kwa kulenga vituo vya nishati hali ambayo itayumbisha zaidi masoko ya nishati na fedha duniani na wakati huo huo kuzidisha mgogoro wa kikanda.
Rais wa Marekani Donald Trump, ameonya kwamba nchi yake itaishambulia na kuiharibu kabisa miundombinu ya nishati ya umeme iwapo Jamhuri hiyo ya kiislamu haitoufungua mlango bahari wa Hormuz katika muda wa saa 48. Tamko la Trump amelitoa siku moja tu baada ya kuzungumzia kuhusu "kuvimaliza" vita, ambavyo sasa viko katika wiki yake ya nne.
Iran ilionya Jumapili kwamba itailenga miundombinu ya Marekani, ikiwemo ya nishati katika eneo la Ghuba, ikiwa Trump atatekeleza vitisho vyake, ambavyo alivitoa huku Wanajeshi wa Marekani na vifaa vya kijeshi vikielekea katika eneo la Mashariki ya Kati.
Zaidi ya watu 2,000 wameuawa mpaka sasa tangu Marekani na Israel zilipoanzisha vita dhidi ya Iran mnamo Februari 28. Vita hivyo vimeathiri masoko ya biashara, vimeongeza gharama za mafuta na kuchochea hofu ya mfumuko wa bei duniani na pia vimeuathiri Muungano wa Magharibi ulioundwa1945 baada ya vita unaoongozwa na Marekani unaounganisha Ulaya Magharibi na Amerika Kaskazini kupitia taasisis kama vilejumuiya ya kujihami ya NATO.
Mchambuzi wa masoko ya Hisa Tony Sycamore, amesema Iran ikivilenga vituo vya nishati kwenye nchi za Saudi Arabia, Falme za Kiarabu na Qatar, hatua hiyo bila shaka itaongeza maumivu kwa kupandisha bei ya nishati na kuziingiza nchi hizo katika mgogoro mpana wa kikanda.
Amesema mashambulizi ya Iran yamesababisha kufungwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz, eneo jembamba linalopitisha takriban theluthi moja ya gesi asilia duniani na mafuta, na kufungwa kwake kumesababisha mgogoro mbaya zaidi wa mafuta tangu miaka ya 1970 na kupanda bei za gesi barani Ulaya hadi asilimia 35 wiki iliyopita.
Mchambuzi wa masoko ya Hisa Tony Sycamore, amesema wazo la Trump kuhusu kuishambulia Tehran kutokana na kuufunga mlango bahari wa Hormuz ni kwa ajili ya kuiadhibu na kuidhoofisha Iran kiuchumi na kisiasa.
Trump na utawala wake wanatoa ujumbe mchanganyiko kuhusumalengo ya Marekani katika kipindi chote cha vita, hatua hiyo inawachanganya washirika wa Marekani wakitafuta majibu bila kuyapata.
Kura mpya ya maoni ya Reuters/Ipsos, iliyofanywa wiki iliyopita, imebaini kuwa asilimia 59 ya Wamarekani hawakubaliani na mashambulizi ya kijeshi ya Marekani dhidi ya Iran, huku asilimia 37 wakiwa wanaunga mkono vita hivyo.
Vita hivyo vimekuwa dhima kubwa ya kisiasa kwa Trump kabla ya uchaguzi wa bunge wa katikati utakaofanyika mwezi Novemba, huku ongezeko la bei ya nishati likichochea mfumuko wa bei nchini Marekani na kuwaathiri vibaya biashara pamoja na watumiaji.