1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tokyo yasema mandalizi ya Olympiki yako pale pale

Deo Kaji Makomba
12 Machi 2020

Wakati dunia ikiwa katika juhudi za kupambana na virusi hatari vya Corona, Tokyo yaendelea na mandalizi ya mashindano ya Olimpiki, licha ya WHO kutangaza rasmi kuwa virusi vya Corona ni janga la kimataifa.

Coronavirus in Japan
Picha: picture alliance/AP Images

Wakati dunia ikiwa katika juhudi za kupambana na virusi hatari vya corona, mji wa Tokyo umeendelea na mandalizi ya mashindano ya Olimpiki licha ya shirika la afya duniani WHO kutangaza rasmi kuwa virusi hivyo ni janga la kimataifa.

12.03.2020 Japan imesema itaendelea na maandalizi yake ya michezo ya olimpiki na ile ya michezo ya Olimpiki kwa walemavu kama ilivyopangwa hapo awali hata baada ya shirika la afya duniani WHO kutangaza rasmi kuwa homa itokanayo na virusi vya corona ni janga la kimataifa.

"Hakuna mabadiliko kutoka kwa msimamo wa serikali na kwamba tutafanya mandalizi kwa ajili ya michezo ya Olimpiki ya Tokyo kama ilivyopangwa hapo awali wakati tukiratibu mashindano hayo kwa ukaribu na kamati ya kimataifa ya Olimpiki, waandalizi wa Tokyo na serikali ya jiji la Tokyo," msemaji wa serikali, Yoshihide Suga, ameumbia mkutano wa wandishi wa habari.

Yoshihide Suga msemaji wa serikali ya JapanPicha: Reuters/F. Robichon

Wajumbe wa kamati ya mandalizi ya Tokyo pia wamesema kuwa mashindano ya Olimpiki yatafanyika kama ilivyopangwa.

"Hakuna chochote ambacho kimebadilika sana. Tunafanya kazi na mashirika yanayohusika na maandalizi ya michezo," afisa mkuu ambaye jina lake halikutajwa aliliambia shirika la habari la Kyodo.

Hata hivyo mwanachama wa kamati kuu ya maandalizi ya mashindano ya Olimpiki, Haruyuki Takahashi, aliliambia shirika la habari la Kyodo Jumatano iliyopita kuwa atapendekeza mashindano ya olimpiki yasogezwe mbele kwa mwaka mmoja au miwili badala ya kufutwa kutokana na janga la kimataifa la virusi vya corona.

Takahashi ameongeza kusema kuwa kucheleweshwa kwa mashindano hayo kwa miaka miwili kutawarahisishia waandaaji kwa sababu ratiba ya mashindano yajayo yamekwishapangwa.

Kamati ya maandalizi ya mashindano hayo ilipinga kuwa na taarifa ya mapendekezo yaliyotolewa na Takahashi.

Tamko la shirika la Afya duniani kuwa suala la virusi vya corona limefikia hatua ya kuitwa janga la kimataifa linakuja ikiwa ni takribani miezi minne na nusu kabla ya kuanza kwa mashindano ya Olimpiki yaliyoratibiwa kuanza Julai 24 mwaka huu.

Takribani wanariadha 11,000 wanatarajiwa kushiriki katika mashindano hayo. Na mashindano ya Olimpiki ya walemavu yanatarajiwa kuanza Agosti 25 mwaka huu huko Tokyo.

Chanzo DPA

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW