Tottenham yamtimua kocha ikiwa ukingoni kushuka daraja
11 Februari 2026
Licha ya kuingoza Tottenham hadi kwenye raundi ya 16 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, Frank amejikuta akikabiliwa na msimu mbaya wa ligi ya nyumbani, Premier.
Kipigo cha 2-1 kutoka kwa Newcastle siku ya Jumanne kiliifanya klabu hiyo kutokuwa na ushindi wowote kwenye mechi za ligi kwa mwaka huu wa 2026.
"Klabu imeamua kuchukua uamuzi wa kumbadilisha kocha wa klabu ya wanaume na Thomas Frank ataondoka leo," Tottenham ilisema kwenye taarifa Jumatano. "Tulimteua Thomas Juni 2025, na tumempa muda na msaada aliouhitaji ili kujenga pamoja mustakabali wa timu."
"Hata hivyo, matokeo na mchezo mbovu vimeifanya bodi kuhitimisha kwamba kunahitajika mabadiliko na hasa katika kipindi hiki cha msimu."
Nafasi wazi Spurs
Kuondoka kwa Frank kunamaanisha Spurs sasa inasaka kocha mpya wa sita katika kipindi cha chini ya miaka 7 tangu Mauricio Pochettino alipoondoka 2019.
Mdenmark huyo alipokea kijiti kutoka kwa Ange Postecoglou mwishoni mwa msimu uliopita, aliyefukuzwa licha ya kuiongoza Spurs hadi kushinda kombe la kwanza baada ya miaka 17, pale iliposhinda Ligi ya Europa dhidi ya Manchester United na kisha kufuzu kwenye michuano ya Mabingwa Ulaya.
Lakini Frank, licha ya kufanikiwa sana akiwa na Brentford, hakuweza kuonyesha makali hayo alipohamia Tottenham, ambako ameshinda michezo michezo 7 tu kati ya 26 ya ligi.
Spurs ilishinda mara ya mwisho Disemba 28 ikiwa nyumbani dhidi ya Newcastle, na kukata ukame wa mabao baada ya mechi 11 kwenye ligi hiyo kuu ya England. Hivi sasa klabu hiyo iko nafasi ya 16 kwenye msimamo wa ligi, nafasi mbili kabla ya mstari wa kushuka daraja.