TRIPOLI: Baraza la mahakama kuu kutoa uamuzi
16 Julai 2007Matangazo
Baraza la mahakama kuu nchini Libya leo linatarajiwa kutoa uamuzi dhidi ya hukumu ya kifo inayowakabili wauguzi watano raia wa Bulgaria na daktari mmoja wa Kipalestina.
Watalaamu hao wa afya walihukumiwa baada ya kupatikana na hatia ya kuwaambukiza kwa makusudi virusi vya UKIMWI watoto 430 mnamo mwaka 1999.
Wakfu ulioanzishwa kwa niaba ya familia za watoto hao umekubali kupokea fidia ya takriban dola millioni 460 hatua ambayo inafungua mlango wa kulainisha adhabu kali inayowakabili wauguzi hao.
Iwapo wauguzi hao watapunguziwa hukumu na kupata adhabu ya kifungo badala ya kunyongwa, umoja wa ulaya unapendekeza kuwa adhabu hiyo waitumikie katika jela za bara Ulaya.