Trump ahusisha kuikosa Nobel na msimamo juu ya Greenland
20 Januari 2026
Kwenye ujumbe mfupi wa maandishi aliomtumia Waziri Mkuu wa Norway, Jonas Gahr Støre, siku ya Jumatatu (Januari 19), Trump alisema haoni tena ana "wajibu wa kufikiria amani pekee".
Ujumbe huo unaonekana kuzungumzia moja kwa moja mpasuko uliozuka kati ya Washington na washirika wa karibu wa Ulaya kutokana na kitisho cha Trump anayetaka kukichukuwa kisiwa cha Greenland ambacho kinamilikiwa na Denmark, iliyo mwanachama wa muuungano wa kijeshi wa NATO.
Siku ya Jumamosi (Januari 17), Trump alitangaza ongezeko la ushuru wa asilimia 10 kuanzia Februari Mosi kwa bidhaa za mataifa manane ya Ulaya yanayoziunga mkono Greenland na Denmark, ikiwemo Norway.
Mkuu wa Sera za Nje wa Umoja wa Ulaya, Kaja Kallas, alisema ingawa Umoja huo "hautaki vita, lakini hauyumbi kwenye msimamo wake" dhidi ya uamuzi huo wa Trump wa kuitwaa Greenland.