1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump ahusisha msimamo kuhusu Greenland na kukosa Nobel

20 Januari 2026

Rais wa Marekani Donald Trump amehusisha msimamo wake mkali kuhusu Greenland na kushindwa kupata Tuzo ya Amani ya Nobel. Kauli hiyo imeongeza mvutano kati ya Marekani, Ulaya na washirika wa NATO.

Picha muunganiko I Trump - Greenland
Rais Trump anadai dunia haiwezi kuwa na amani bila ya Marekani kuidhibiti kikamilifu Greenland.Picha: Federico Parra/Odd Andersen/AFP

Rais wa Marekani Donald Trump ameibua taharuki mpya baada ya kuhusisha msimamo wake mkali kuhusu Greenland na kutopata Tuzo ya Amani ya Nobel. Kauli hiyo imetafsiriwa kama ishara ya mabadiliko makubwa katika sera zake za kimataifa.

Katika ujumbe wa maandishi uliotolewa kwa serikali ya Norway, Trump alisema hahisi tena wajibu wa kufikiria amani pekee. Alidai kuwa kunyimwa Nobel kulibadilisha mtazamo wake.

Trump alimtumia ujumbe huo Waziri Mkuu wa Norway, Jonas Gahr Støre. Ujumbe huo uliibua mjadala mpana barani Ulaya na Marekani.

Kauli hizo zimeongeza mvutano uliokuwepo kuhusu Greenland. Marekani imekuwa ikitoa vitisho vya kuchukua udhibiti wa kisiwa hicho, hata ikibidi kwa nguvu.

Greenland ni eneo linalojitawala chini ya Denmark na ni mwanachama wa NATO. Washirika wengi wa Ulaya wamekataa vikali madai ya Trump.

Wakaazi wa Greenland wakiandamana mbele ya ubalozi mdogo wa Marekani wakiwa na mabango yenye ujumbe usemawo eneo hilo haliuzwi.Picha: Christian Klindt Soelbeck/Ritzau Scanpix/IMAGO

Ulaya yasisitiza Greenland haiuzwi

Nchi kadhaa za Ulaya zilitangaza mshikamano wao na Denmark, na kusisitiza kuwa kisiwa hicho kikubwa zaidi duniani hakiuzwi. 

Umoja wa Ulaya ulisema hautafuti ugomvi na Marekani. Hata hivyo, uliahidi kusimama imara kulinda misingi ya kimataifa.

Trump alitangaza ushuru wa asilimia 10 kwa bidhaa kutoka mataifa nane ya Ulaya alioyataja kupingana na azma yake ya kuitwaa Greenland. Alisema hatua hiyo ni sehemu ya shinikizo la mazungumzo.

Hatua hiyo ilitafsiriwa kama kisasi cha kisiasa. Ulaya ilianza kuandaa mikakati ya kulipiza ushuru.

Wakati huo huo, maandamano makubwa yalifanyika Greenland. Wakazi walipinga wazi jaribio lolote la kuchukuliwa kwa kisiwa chao.

Trump asisitiza Denmark haiwezi kulinda Greenland

Waziri Mkuu wa Greenland Jens-Frederik Nielsen alisema vitisho havitabadilisha msimamo wao. Alisisitiza haki ya kujitawala na kuheshimiwa.

Mawaziri wa Ulaya walieleza kuwa wanajeshi waliotumwa Greenland walikuwa wa mfano tu. Lengo lilikuwa kutathmini usalama wa Aktiki.

Trump hata hivyo alipuuzilia mbali hoja hiyo. Alisema NATO imekuwa ikionya Denmark kuhusu hatari za Urusi na China.

Katika mitandao ya kijamii, Trump alichapisha picha zilizobadilishwa. Picha hizo zilionyesha Greenland kama eneo la Marekani.

Hatua hizo zilionekana kama uchokozi wa wazi. Wakosoaji walisema zinachochea mivutano isiyo ya lazima.

Waziri Mkuu wa Greenland, Jens-Frederik Nielsen, akizungumza wakati wa maandamano dhidi ya sera ya Trump kuhusu Greenland mbele ya ubalozi mdogo wa Marekani mjini Nuuk, Greenland, Jumamosi, Januari 17, 2026.Picha: Evgeniy Maloletka/AP Photo/picture alliance

'Greenland kunufaika chini ya udhibiti wa Marekani'

Katika ujumbe mwingine, Trump alisema dunia haitakuwa salama bila udhibiti kamili wa Marekani kwa Greenland. Kauli hiyo ilishtua diplomasia ya kimataifa.

Ikulu ya White House ilithibitisha ujumbe huo. Ilisema Trump anaamini Greenland itanufaika chini ya ulinzi wa Marekani.

Norway ilijibu kwa kusisitiza uhuru wa Denmark. Ilikumbusha kuwa Tuzo ya Nobel hutolewa na kamati huru.

Trump amekuwa akitamani tuzo hiyo kwa muda mrefu. Mwaka jana ilitolewa kwa mwanaharakati wa upinzani wa Venezuela.

Hivi karibuni Trump alisema hajali tena kuhusu Nobel. Alidai lengo lake ni "kuokoa maisha”.

Kitisho cha jumuiya ya NATO

Wachambuzi wanasema mgogoro huu unaweza kutishia kuisambaratatisha jumuiya ya NATO. Tayari muungano huo ulikuwa na changamoto kutokana na vita vya Ukraine.

Masoko ya kifedha barani Ulaya yameathirika. Wawekezaji wanaogopa kurejea kwa vita vya kibiashara.

Wanajeshi wa Denmark wakishiriki mafunzo ya kutumia risasi halisi baada ya kuwasili Greenland, Jumapili, tarehe 18 Januari 2026.Picha: Danish Defence Command/UPI Photo/picture alliance

Viongozi wa EU wanapanga mkutano wa dharura Brussels. Wanajadili ushuru na hatua za kupambana na shinikizo.

Mkutano wa Jukwa la Dunia la Kiuchumi wa Davos unatajwa kama fursa ya mazungumzo. Trump anatarajiwa kukutana na viongozi kadhaa.

Hata hivyo, wasiwasi bado ni mkubwa. Swali kuu ni kama diplomasia itashinda au mvutano utaendelea kuongezeka.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW