1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump aanza ziara ya siku nne Mashariki ya kati

13 Mei 2025

Rais wa Marekani Donald Trump ameanza ziara yake Mashariki ya kati. Ameanzia Riyadh, Saudi Arabia. Anatazamiwa kujikita kwenye mazungumzo kuhusu uchumi, mpango wa nyuklia wa Iran na kuvimaliza vita Ukanda wa Gaza.

Trump yuko Marekani kwa ziara ya siku nne
Rais wa Marekani Donald Trump na Mwanamfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin SalmanPicha: Alex Brandon/AP Photo/picture alliance

Baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mfalme Khalid, Donald Trump amepokelewa na Mwanamfalme Mohammed bin Salman, aliyemuhakikisha kwamba Saudi Arabia itabakia kuwa mshirika wake imara.

Kama sehemu ya kuonesha heshima, ndege za kijeshi za Saudi Arabia zilionekana zikiisindikiza ndege ya Rais wa Marekani Airforce One ilipokaribia mji mkuu Riyadh.

Soma zaidi: Nchi za Kiarabu zatumaini biashara na Marekani licha ya vita vya Gaza

Trump na Mwanamfalme bin Salman wameandaliwa kushiriki chakula cha mchana katika dhifa maalumu sambamba na wafanyabiashara wakubwa walioalikwa wakiwemo Mkurugenzi mkuu wa Kampuni ya Blackstone Stephen Schwarzman, Larry Fink wa BlackRock na Elon Musk.

Anatarajiwa pia kufanya mkutano wa uwekezaji kati ya Marekani na Saudi Arabia kabla ya kuelekea Umoja wa Falme za Kiarabu na Qatar katika ziara yake ya siku nne kwenye mataifa hayo ya ghuba.

Viongozi wa Kuwait, Oman na Bahrain kukutana na Trump

Kando ya viongozi wa Saudia, kesho Jumatano kiongozi huyo wa Marekani anatazamiwa kukutana na viongozi wa Kuwait, Oman na Bahrain. Mazungumzo yake mjini Riyadh yanayotazamiwa kulenga zaidi mikataba ya kibiashara kuliko masuala ya kidiplomasia huenda yakazaa matunda kwa kupata makubaliano na Saudi Arabia kuhusu teknolojia ya nyuklia.

Rais wa Marekani Donald Trump baada ya kuwasili Riyadh 13.05.2025Picha: Alex Brandon/AP Photo/picture alliance

Nchi hiyo tayari imeshatangaza kuwa itawekeza dola za Kimarekani bilioni 600 nchini Marekani katika miaka ijayo wakati  Trump amesema atamwomba Mwanamfalme Salman kiasi hicho kiongezwe hadi kufikia dola trilioni moja.

Saudi Arabia ilikuwa pia nchi ya kwanza kwa Trump kuitembelea alipoingia madarakani katika awamu yake ya kwanza mnamo mwaka 2017  baada ya nchi hiyo  yenye utajiri mkubwa wa mafuta kutangaza kuwekeza dola bilioni 450 Marekani.

Wakati suala la mpango wa nyuklia ya Iran likitarajiwa kuwa katika orodha ya ajenda za mazungumzo ya Trump katika ziara hiyo, Iran imetoa onyo. Kituo cha habari cha Nournews cha nchini humo kimemnukuu mkuu wa utumishi katika jeshi Mohammad Bagheri akisema Saudi Arabia inapaswa kutokuegemea upande wowote. Ameongeza kuwa uchokozi wowote dhidi ya Iran kwa hakika utasababisha Iran ilipe kisasi.

 

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW