Trump: Makubaliano ya Greenland yamefurahiwa na kila mmoja
22 Januari 2026
Trump ameyasema hayo wakati ambapo pia amedai kuwa hatotumia nguvu kukichukua kisiwa cha Greenland na pia kudai kuwa hatoziwekea tena ushuru bidhaa za mataifa nane ya Ulaya yaliyokuwa yanaupinga mpango wake wa kuitwaa Greenland.
Akizungumza na kituo cha habari cha Marekani CNBC,Trump amesema makubaliano hayo ni ya muda mrefu na kila mmoja ameyafurahia ila hakutoa taarifa zaidi na hakusema pia iwapo hiyo inamaanisha kuwa Marekani itakuwa na udhibiti wa kisiwa hicho cha eneo la Arctic.
Tahadhari ya matumaini ya mapema
Trump ameyasema yote hayo baada ya mkutano huko Davos na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO Mark Rutte ambaye kupitia msemaji wake, ameyathibitisha hayo aliyoyasema Trump.
Lakini waziri wa fedha wa Ujerumani Lars Klingbeil ameonya dhidi ya kuwepo kwa matumaini ya mapema kutokana na hiyo kauli ya Trump kuwa sasa hatoziwekea tena bidhaa za Ulaya ushuru.
Vitisho vya Trump vilikuwa vimezusha mmojawapo wa mizozo mikubwa zaidi katika eneo la transatlantic kuwahi kushuhudiwa kwa miongo kadhaa, akisema kwamba anaweza kuisambaratisha NATO.
Denmark yakaribisha nguvu kutotumiwa
Lakini sasa Waziri Mkuu wa Denmark Dick Schoof amesema kuwa Marekani na Ulaya kwa sasa ziko katika njia ya kusuluhisha tofauti zao.
Waziri wa mambo ya kigeni wa Denmark Lars Lokke Rasmussen naye ameikaribisha hatua ya Trump kutotumia nguvu katika azma yake ya kutaka kuichukua Greenland ila ameonya kuwa rais huyo wa Marekani ana malengo ambayo hawawezi kuyakubali.
Kabla Trump kutangaza mabadiliko hayo ya kimsimamo kuhusu Greenland, serikali ya kisiwa hicho ilikuwa imewapa ushauri raia wake kuhusiana na hatua za kuchukua endapo kutakuwa na "mzozo" nchini humo.
Vyanzo: AFP/DW