Tymoshenko atibiwa na madaktari wa Ujerumani
5 Mei 2012Zoezi hilo la tiba kamili linatarajia kuanza wiki ijayo chini ya timu ya madaktari hao wa Ujerumani. Hali ya afya ya mama huyo imezusha wasiwasi miongoni mwa jumuiya za kimataifa huku Sweden ikijiunga siku ya Ijumaa katika mgomo wa kutaka nchi hiyo itolewe katika orodha ya mataifa yatakayoandaa michezo ya bara la Ulaya ya mwaka 2012 ikishirikiana na Poland.
Karl Max Einhaeupl, Mkuu wa hospital ya mjini Berlin pamoja na mtaalamu wa upasuaji wa hospitali hiyo Norbert Haas wamemfanyia uchunguzi Tymoshenko katika jela ya mjini Kharkiv anakotumikia kifungo kilometa 410 kutoka mji mkuu wa nchi hiyo Kiev. Madaktari wa Ukraine pamoja na wanadiplosia wa Ujerumani walikuwepo wakati uchunguzi huo unafanyika.
Mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 51 amepata majeraha mgongoni. Alianza mgomo wa kutokula chakula mwishoni mwa mwezi Aprili akipinga mateso aliyoyapata kutokana na kipigo alichopata kutoka kwa askari wa jela aliyomo wakati anapelekwa hospitali.
Inaripotiwa kuwa kwa sasa hawezi kuongea bila msaada. Binti wa mwanasiasa huyo amesema kuwa hali ya kiafya ya mama yake imezidi kudhoofika katika siku za hivi karibuni huku serikali ya nchi hiyo ikisema kuwa haitamlazimisha kula.
Hali ya mama huyo imekuwa alama ya pingamizi kwa viongozi wa bara la Ulaya ambao wamesusia mkutano na nchi hiyo na kupinga maandalizi yake katika michezo barani humo mwezi June mwaka 2012. Waziri Mkuu wa Sweden Fredrik Reinfeldt amekiambia kituo cha Televisheni cha STV nchini mwake kuwa hatahudhuria mechi za timu ya taifa ya nchi yake zitakazochezwa nchini Ukraine.
Rais wa Umoja wa Ulaya Herman Van Rompuy ambaye amekutana na Reinfeldt siku ya Ijumaa, amesema kuwa hakupanga kuhudhuria michezo hiyo hapo kabla kwa kuwa nchi yake Ubelgiji haishiriki katika fainali hizo.
Hata hivyo Rompuy amesema kuwa Umoja wa Ulaya umekataa kukutana na viongozi wa Ukraine mjini Brussels mkutano ambao ulikuwa ni muhimu zaidi kisiasa kuliko kuhudhuria ama kutohudhuria fainali hizo za Mataifa ya Ulaya nchini humo.
Reinfeldt amesema kuwa analiona suala la Tymoshenko kuwa ni jambo lenye umuhimu wa hali ya juu na kusema kuwa haki za binaadamu na utawala wa sheria haviheshimiwi.
Siku ya Alhamis, Makamishna 27 wa nchi mwanachama wa Umoja wa Ulaya na Rias wa Romania walijiunga na orodha ya watu wanaoipinga Ukraine waziwazi kuhusu suala la Tymoshenko. Haijajulikana wazi hadi sasa kama Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na mawaziri wake watahudhuria michezo hiy nchini Ukraine.
Maafisa wa Ukraine wamekanusha madai kuwa Tymoshenko aliteswa kwenye jela aliyomo na kuwa majeraha aliyonayo hakuyapata wakati anasafirishwa kwenda hospitali tarehe 20 mwezi Aprili. Mwendesha Mashitaka wa nchi hiyo Viktor Pshonka amesema kuwa huenda mama huyo alijitia majeraha mwenyewe. Mwanaisa huyo ambaye ni mpinzani mkuu wa Rais Viktor Yanukovych yupo katika kifungo cha miaka saba jela tangu mwaka uliopita kwa makosa ya matumizi mabaya ya madaraka.
Mwandishi: Stumai George
Mhariri: Sekioni Kitojo