Uchaguzi wapuuziwa na wapinzani Syria
8 Mei 2012Akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa Ban kwa mara nyingine amelaani vitendo vya mauwaji ya kinyama vinavyofanywa na majeshi ya Rais Bashar al-Assad, lakini pia amesema mashambulizi ya upinzani pia yanaendeleza uovu.
Kiongozi huyo aliendelea kwa kusema hivi sasa wanashindana na wakati katika kudhibiti kutokea kwa vita kamili vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo, wakati ambapo idadi ya vifo ikizidi kuongezeka.
Kwa ujumla, Umoja wa Mataifa kwa sasa unakadiria kiasi ya watu 9,000 wameuwawa tangu kuanza kwa vuguvugu la kutaka kumuondoa madarakani rais Assad miezi 14 iliyopita, huku makundi ya haki za binadamu yakisema waliokufa wamefikia watu 11,000.
Akizungumza na kamati maalum ya baraza la hilo la usalama mjini Washington, katibu huyo mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema vikosi vya serikali vinaendelea kufanya ukandamizaji dhidi ya raia na kwamba kila kukicha kunaonekana taswira nyingine nchini Syria.
Amesema hali inayojidhihirisha ni kwamba vikosi vinaonekana vikichoma moto katikati ya miji, raia wasio na hatia wanauwawa na hata watoto wadogo huku wengine wakikamatwa na kuteswa kinyama.
Pamoja na hayo, katibu mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa ameshutumu kufanyika kwa uchanguzi wa bunge hapo jana, wakati vurugu zikiendelea pamoja na kushindwa kuhusisha upande wa upinzani.
"Kwa namna gani unaweza kuendesha uchaguzi wakati nusu ya taifa kuna mapigano na majeshi yanashambulia kwa mabomu miji na majiji"
Waangalizi nchini humo wanasema kiasi ya watu 25 wameuwawa wakati ambapo uchaguzi huo ukiendelea hapo jana.
Katika kauli ya Ban Ki-moon kupitia msemaji wake, Martin Nesirky, inasistiza kwamba "ni kwa mazungumzo thabiti yenye kushirikisha pande zote muhimu ndipo suluhu ya kweli itapatikana nchini Syria".
Kamati ya kusimamisha mapigano inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa ambayo ilianza kazi Aprili 12 imeshindwa kufanikisha usitishaji wa mapigano na kwamba pande zote mbili nchini humo zikishutumiwa kwa kukiuka makubaliano ya amani.
Katika upande mwingine, serikali ya Lebanon imefanikiwa kuikamata meli moja iliyokuwa na shehena ya silaha kali za kivita. Chanzo cha habari kinasema silaha hizo zikuwa zimehifadhiwa kwenye gari mbili zilizokuwa ndani ya meli hiyo.
Hata hivyo, chanzo cha habari hakikusema wapi ambapo meli hiyo ilikuwa imetia nanga katika bandanri moja iliyopo kaskazini mwa Lebanon inaelekea lakini Syria imekuwa ikisema mara kadhaa kwamba silaha zimekuwa zikiiingizwa nchini humo kupitia mpaka wake na Lebanon pamoja na nchi nyingine kwa ajili ya kuwasaidia waasi.
Mwandishi: Sudi Mnette
Mhariri:Miraji Othman