1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani, Ufaransa kuanzisha baraza la pamoja la usalama

7 Mei 2025

Ujerumani na Ufaransa zimekubaliana kuunda baraza la pamoja la ulinzi na usalama. Tangazo kuhusu uamuzi huo limetolewa na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron wakati wa ziara ya Kansela mpya wa Ujerumani Friedrich Merz.

Ujerumani na Ufaransa zimekubaliana kuanzisha baraza la pamoja la usalama
Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron Mei 07, 2025Picha: Sean Gallup/Getty Images

Ziara hiyo ni ya kwanza kwa Kansela huyo wa Ujerumani tangu alipoingia mamlakani Jumanne 06.05.2025. Nchi hizo mbili zimefanya makubaliano hayo ya kuunda baraza la usalama litakalokutana mara kwa mara kama sehemu ya juhudi za kuongeza uwekezaji katika ulinzi. Makubaliano hayo yamefikiwa huku Ulaya ikifanya juhudi za kuimarisha ulinzi wakati Ukraine ikikabiliwa na vita dhidi ya Urusi.

Soma zaidi: Friedrich Merz afanya ziara yake ya kwanza Ufaransa na Ujerumani

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amefafanua zaidi kuhusu makubaliano hayo na kusema, "Tutaharakisha programu zetu za Ujerumani na Ufaransa na kuimarisha uwezo wetu. Mbali na mizinga, ndege za kivita na makombora ya masafa marefu, tutaanzisha baraza la usalama litakalotoa majibu ya kiutendaji kwa changamoto zetu za kimkakati."

Zaidi Macron ameeleza kuwa nchi hizo mbili zinataka kufanya kazi pamoja katika mambo zinayoyapa kipaumbele yakiwemo uhuru, ulinzi na ushindani huku akisisitiza kuwa jukumu kubwa kabisa la Ufaransa na Ujerumani ni kudumisha ulinzi barani Ulaya.

Ushirikiano kuelekezwa pia kwenye uchumi, na fedha

Kwa upande wake Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz  amesema nchi yake na Ufaransa zitaongeza pia ushirikiano katika maeneo mengine kadhaa. Merz ameeleza kuwa, "Ninataka kuweka wazi kuwa serikali zetu zinachukua majukumu ya pamoja, yakiwemo katika kazi ambayo tayari inafanyika kwenye wizara tofauti. Tutaongeza juhudi katika maeneo yote kama vile katika sera ya uchumi, kwenye sera ya usalama, ulinzi na ya fedha ili kuziimarisha"

Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz katika ziara yake ya kwanza nchini Ufaransa Mei 07.2025Picha: Sean Gallup/Getty Images

Ameyasema hayo akiwa sambamba na Rais Macron na kuongeza kuwa nchi zote wanachama wa Umoja wa Ulaya zinapaswa kuongeza bajeti zao za ulinzi ili kuziba mwanya katika uwezo wa jumuiya hiyo na kuendelea kuiunga mkono Ukraine.

Soma zaidi: Merz afanya ziara ya kushtukiza Paris kwa mazungumzo na Macron

Baada ya kukutana na Macron, Merz anaelekea nchini Poland atakapokutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu Donald Tusk. 

Ameanza siku yake ya kwanza kazini kwa kufanya ziara katika mataifa hayo mawili wakati Ulaya ikifanya jitihada za kuongeza uwezo wake wa kujilinda kukiwa pia na mashaka kuhusu dhamira ya Marekani kwa usalama wa Ulaya. Hata hivyo ameseisitiza kuwa makubaliano yoyote ya amani ya Ukraine yanahitaji Marekani ishirikishwe.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW