1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUfaransa

Wafaransa waandamana kupinga hatua za rais Macron

10 Septemba 2025

Wakati Waziri Mkuu mpya wa Ufaransa Sebastien Lecornu akichukua rasmi wadhifa huo Jumatano (10.09.2025), waandamanaji wameingia mitaani kudhihirisha kutoka mashinani kwamba wanapinga hatua za Rais Emmanuel Macron.

Montpellier 2025 | Maandamano ya kupinga hatua za Rais Macron
Maandamano nchini Ufaransa yakipinga hatua za kisiasa za rais Emmanuel MacronPicha: Manon Cruz/REUTERS

Sébastien Lecornu , aliyechaguliwa na Rais Emmanuel Macron kuwa waziri mkuu wa tano wa Ufaransa katika kipindi cha miaka miwili, alikabidhiwa ofisi ya Matignon na Waziri Mkuu anaeondoka Francois Bayrou, ambaye serikali yake iliangushwa baada ya kushindwa kura ya imani Bungeni.

Lecornu mwenye umri wa miaka 39, ambaye alikuwa waziri wa ulinzi na mwanasiasa mtiifu kwa  Macron , amechukua usukani wakati maandamano yakiongozwa na kikundi cha mrengo wa kushoto yakishuhudiwa sehemu mbalimbali huko Ufaransa chini ya kauli mbiu ya "kuzuia kila kitu".

Maandamano hayo yameshuhudiwa katika miji mbalimbali ikiwa ni pamoja na mji mkuu Paris, Lyon, Bordeaux, Marseille na kwengineko. Takriban maafisa wa polisi 80,000 wamesambazwa kote Ufaransa huku waandamanaji wakiweka vizuizi kwa kutumia mapipa ya taka, mabango na hivyo kuzuia barabara na kuvuruga huduma muhimu kama usafiri na shule.

Waandamanaji zaidi ya 200 wakamatwa

Polisi wa Ufaransa wakijiandaa kukabiliana na waandamanaji huko NantesPicha: Stephane Mahe/REUTERS

Waziri wa Mambo ya Ndani wa  Ufaransa  anayeondoka Bruno Retailleau amesema maandamano ya vurugu hayatovumiliwa na kutangaza kuwa tayari watu karibu 250 wamekamatwa. Waandamanaji wanapinga vikali uamuzi wa Macron wa kumteua mshirika wake wa karibu kuwa waziri mkuu wakilalamika kuwa wanahitaji mabadiliko.

Macron alimteua Lecornu jana jioni, siku moja baada ya mtangulizi wake Francois Bayrou  kupoteza kura ya imani yake bungeni kufuatia jaribio lake la kutaka kupitisha bajeti iliyopingwa vikali na wabunge na ambayo ilijikita zaidi katika kubana matumizi hadi dola bilioni 52 ili kupunguza deni la Ufaransa.

Lecornu aahidi kuja na sera mpya

Waziri Mkuu mpya wa Ufaransa Sebastien Lecornu akiwa katika Ikulu ya Elysée mjini ParisPicha: Gao Jing/Xinhua/picture alliance

Lecornu anayekuwa waziri mkuu wa saba tangu Macron aingie madarakani mwaka 2017 na wa tatu ndani ya muda wa mwaka mmoja pekee amesema atalihutubia taifa katika siku zijazo ili kuelezea sera zake, akiahidi kuwa zitakuwa na utofauti mkubwa na zile zilizopita:

" Kimsingi tunapaswa kukomesha hali hii ya kutozingatia uhalisia: Hasa huu wa utofauti kati ya hali ya kisiasa na kile ambacho raia wenzetu wanachokitarajia katika maisha yao ya kila siku, uhalisia wa hali ya kiuchumi na kijamii na kwa usalama wao. Kwa ufupi, hili ndilo jukumu kuu tulilopewa."

Maandamano haya mapya yaliyoibuka sehemu mbalimbali nchini Ufaransa, yanakumbushia vuguvugu dhidi ya serikali lililofahamika zaidi kwa kifaransa kama "Gilets-Jaune" yaani  vizibao vya Njano  ambalo liliibuka mwaka 2018 bila ya kuwa na uongozi ulio wazi lakini lililoibua changamoto kubwa kwa Macron wakati wa muhula wake wa kwanza madarakani.

// AFP, DPA, AP

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW