Uhamiaji usiofuata taratibu washuka kwa nusu Ujerumani
2 Januari 2026
Idadi ya wahamiaji wanaoingia nchini Ujerumani kinyuem cha sheria imepungua kwa nusu katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na kitengo cha polisi ya mpakani jana Alhamisi.
Katika mwaka wa 2025 Polisi ilirekodi wahamiaji 62,526 wasiofuata utaratibu, kupitia mipaka ya nchi kavu, angani na baharini.
Idadi hiyo ni pungufu ikilinganishwa na wahamiaji 83,572 mwaka 2024 na 127,549 mwaka 2023, ambapo kwa baadhi ya miezi idadi ilivuka 20,000. Mwezi Desemba pekee, takwimu zilishuka hadi chini ya 4,600.
Tangu Septemba 2024, Ujerumani ilirejesha udhibiti wa mipaka yote ya nchi kavu ili kudhibiti uhamiaji haramu. Hatua hizo ziliongezwa nguvu mwezi Mei na Waziri wa Mambo ya Ndani Alexander Dobrindt, baada ya Kansela Friedrich Merz kuingia madarakani.
Tangu wakati huo, polisi wa mpakani wameelekezwa kuwarejesha waomba hifadhi, isipokuwa makundi maalum kama wagonjwa na wanawake wajawazito.
Kimsingi udhibiti wa mipaka hauruhusiwi ndani ya kanda ya usafiri huru ya Schengen, ambayo inahusisha mataifa mengi zaidi ya Umoja wa Ulaya, pamoja na Iceland, Liechtenstein, Norway na Uswisu, isipokuwa katika mazingira ya kipekee, ikiwemo vitisho vya usalama na migogor ya umma.