1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUingereza

Uingereza yaandaa mapokezi makubwa kwa Trump

16 Septemba 2025

Uingereza inamtandikia zulia jekundu Rais Donald Trump wa Marekani katika mapokezi ya heshima kwa kiongozi huyo anayewasili siku ya Jumanne kwa ziara ya pili ya kihistoria kwenye taifa hilo mshirika wa jadi.

Uingereza London 2019 | Donald Trump na Mfalme Charles III
Picha ya Rais Donald Trump wa Marekani (kulia) akiwa na Mfalme Charles III wa Uingereza wakati wa ziara ya Trump jijini London mwaka 2019.Picha: Victoria Jones/AP Photo/picture alliance

Ratiba ya mapokezi ilionesha ulinzi mkali tangu kuwasili kwake mpaka kuhudhuria kwenye tafrija ya chakula cha jioni akiwa ameandamana na Mfalme Charles wa Tatu, lakini ni wazi kuwa upinzani dhidi ya Trump, mwenye umri wa miaka 79 na ambaye mama yake ametokea Scotland, utajitokeza hata kabla ya ziara hiyo. 

Maelfu ya watu walitarajiwa kujipanga kwenye njia ambazo msafara wa Trump  na Mfalme Charles ungelipita wakipaza sauti na kuonesha mabango ya kupinga siasa za Trump ulimwenguni. 

Polisi ya Thames Valley ilisema imetuma kikosi chake maalum kuzunguka Kasri la Windsor anakofikia Trump kama sehemu ya hatua pana za kiusalama, na kwamba kikosi hicho kinajumuisha askari wa kawaida na askari kanzu. 

Ofisi ya Waziri Mkuu wa Uingereza, Downing Street, ilisema kwenye taarifa yake kwamba ziara hiyo ya Trump ingelithibitisha jinsi urafiki usioyumba baina ya nchi hizo mbili ulivyofikia viwango vya juu kabisa.

Mikataba ya mabilioni

Pande hizo mbili zilitazamiwa kusaini msururu wa mikataba yenye thamani ya hadi paundi bilioni 10, ukiwemo ule wa kuharakisha miradi ya nyuklia na pia ule maafisa wa Uingereza wanaouita "ubia wa teknolojia unaongoza duniani".

Kwenye picha hii iliyopigwa wakati wa ziara ya kwanza rasmi ya Donald Trump (wa pili kulia) nchini Uingereza mnamo Juni 2019, anaonekana akiwa na Mfalme Charles III (wa pili kushoto) na wake zao, Melania Trump (kulia) na Malkia Camilla (kushoto).Picha: Chris Jackson/empics/picture alliance

Kuelekea ziara hiyo ya Jumanne (Septemba 16), tayari kampuni ya Google ilishasema kwamba ingeliwekeza kiasi cha paundi bilioni 5 nchini Uingereza ndani ya kipindi cha miaka miwili ijayo, huku kampuni nyengine za Marekani, zikiwemo za PayPal na Citi Group, zikitangaza uwekezaji wa paundi bilioni 1.25.

Mbali na utiaji saini mikataba hiyo, suala la vita vya Urusi nchini Ukraine lilitazamiwa kuchukuwa nafasi kubwa ya mazungumzo kati ya Trump na Waziri Mkuu wa Uingereza , Keir Starmer. 

Starmer ni miongoni mwa viongozi wa Ulaya ambao wamekuwa wakimshinikiza Trump kuendelea kuiunga mkono Kiev, wakihofia kwamba kiongozi huyo wa Marekani anaelemea zaidi upande wa Rais Vladimir Putin wa Urusi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, alisema siku ya Jumanne kwamba kulikuwa na uwezekano Trump kukutana na Rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine wiki ijayo na kwamba bado alikuwa na matumaini ya kufanikisha makubaliano ya amani kati ya Kiev na Moscow.

Kwa upande wake, mke wa Trump, Melania, ambaye anaambatana na mumewe kwenye ziara hii, alionekana kuwa na ratiba tafauti. 

Alitazamiwa kushirikiana na Malkia Camilla, ambaye anaendelea kupana ahuweni baada ya kusumbuliwa na maradhi yaliyomfanya ashindwe kuhudhuria mazishi ya mtawala wa Kent siku ya Jumanne.
 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW