Ujenzi wa makazi mapya ya walowezi wa Kiyahudi usitishwe
13 Desemba 2007JERUSALEM:
Majadiliano ya kwanza ya amani baada ya miaka saba,kati ya wasuluhishi wa Kiisraeli na Kipalestina yamemalizika bila ya makubaliano.Tume ya Wapalestina iliyoongozwa na Waziri Mkuu wa zamani Ahmed Qurei,imeitaka Israel isitishe mipango yake ya kujenga makazi mapya ya walowezi wa Kiyahudi katika Jerusalem ya Mashariki.
Kwa upande mwingine,Waziri wa Mambo ya Nje wa Israel,Tzipi Livni alitoa mwito kwa Wapalestina kuzingatia hofu za Israel kuhusu usalama wake. Ingawa majadiliano hayo hayakuwa na matokeo thabiti,msemaji wa serikali ya Israel alisema, Israel ipo tayari kutafuta njia ya kuafikiana na Wapalestina.Mkutano wa siku ya Jumatano ulilenga kuweka misingi ya majadiliano yanayohusika na masuala ya mipaka na hatima ya mji wa Jerusalem pamoja na wakimbizi wa Kipalestina.