1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaipa Tanzania bilioni 78 kusaidia miradi ya maji

16 Julai 2025

Serikali ya Ujerumani imetoa msaada wa Shilingi bilioni 78.58 za Kitanzania kwa ajili ya kupiga jeki miradi ya maji na maliasili nchini Tanzania, hatua inayotajwa na wanufaika kuwa na faida kubwa kwao.

Tanzania Serengeti
Ujerumani yaipatia Tanzania mabilioni ya yuro ili kupiga jeki miradi ya kimaendeleoPicha: K. Wothe/imageBROKER/picture alliance

Miongoni mwa maeneo yanayotarajiwa kunufaika na msaada huo ni ya kwenye hifadhi za taifa za Serengeti na Katavi ambako uboreshaji wa miundombinu, utoaji elimu pamoja na kuendeleza miradi ya kijamii inayozunguka hifadhi hizo ni sehemu ya vipaumbele vya msaada huo uliotolewa kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW).

Katika eneo la hifadhi ya taifa, utawezesha wataalamu katika maeneo hayo kupata mbinu na uwezo mpya wa kuendeleza utalii na uhifadhi ili kufanya shughuli zote zinazofanywa kwenye maeneo hayo kuwa endelevu.

Nuhu Daniel, ambaye ni msaidizi wa uhifadhi Tanapa, anasema suala la uboreshaji wa barabara ndani ya maeneo ya hifadhi ili kuziwezesha kuwa na uwezo wa kupitika katika kipindi chote cha mwaka ni eneo lingine ambalo limezingatiwa na fedha za msaada huo.

Ujerumani imetoa msaada kwa Tanzania kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani, KFWPicha: Ralph Peters/IMAGO

Vikundi vya maendeleo kunufaika na msaada wa Ujerumani

Vikundi ya maaendeleo pamoja na shughuli za kijamii zinazoendeshwa na wakazi wanaishi kandokando na maeneo ya hifadhi watasaidiwa kwa kupatiwa mikopo kupitia vikundi vyao vinavyofahamika kama benki za maendeo ya kijamii.

Michael Gikaro ambaye ni mwenyekiti wa  mmoja ya vikundi vilivyopo karibu ya eneo la hifadhi anasema mikopo wanayopatiwa imewawezesha kuendesha familia kwa kuanzisha biashara, kupeleka watoto shule na hata kupata matibabu.

Sehemu ya Ziwa Victoria, ambayo serikali ya Ujerumani ilitoa mafungu ya fedha ili kufadhili usambazaji wa maji kutoka kwenye ziwa hiloPicha: danielav212/imago images

Hivi karibuni serikali ya Ujerumani ilitoa mafungu ya fedha ili kufadhili usambazaji wa maji kutoka Ziwa Victoria na kuwafikia wakazi wa maeneo ya kanda ya ziwa waliokuwa wakikabiliwa na adha ya ukosefu wa maji kwa muda mrefu. 

Naibu Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania, Manuel Meuller, anasema shabaha ya mradi huo ni kuziwezesha kaya zaidi katika eneo hilo kunufaika na huduma ya maji safi na salama.

Serikali ya Tanzania inasema mamlaka za maji zimefunguliwa milango kuanzisha miradi ya uendelezaji huduma ya maji, na kulingana na katibu mkuu wizara ya fedha, Dk Natu El-maamry Mwamba mamlaka hizo sasa zinaweza kukopa kwa ajili ya kuendeleza miundombinu ya maji.

Tanzania imekuwa katika kampeni ya kile kinachojulikana "kumtua mama ndoo kichwani" ikimaanisha kumaliza kabisa adha ya ukosefu wa maji ambayo mara nyingi mzigo wake hubebwa na wanawake.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW