1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaonya dhidi ya unyakuzi wa Israel.

10 Juni 2020

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Heiko Maas amesema Ulaya inapinga vikali mipango ya Israel ya kuanza kuyanyakua baadhi ya maeneo kwenye Ukingo wa Magharibi.

Israel Jerusalem Besuch Außenminister Heiko Maas | Pressekonferenz
Picha: Reuters/R. Zvulun

Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza na waziri mwenzake wa Israel, Gabi Ashkenazi.

Ziara ya Maas mjini Jerusalem ambayo ni ya kwanza nje ya Ulaya tangu mripuko wa janga la virusi vya corona, inafanyika wiki chache tu kabla ya Israel kuanza kutanua himaya yake kwa kujenga makazi ya Wayahudi katika Ukingo wa Magharibi, hii ikiwa ni kulingana na mpango tata kuhusu Mashariki ya Kati uliotangazwa na Rais Donald Trump wa Marekani.

Mpango huo ulikabiliwa na ukosoaji mkali kutoka kwa baadhi ya washirika wa karibu kabisa wa Israel, ikiwa ni pamoja na Ujerumani ambayo inasema marekabisho ya ramani ya Mashariki ya Kati yaliyofanywa na upande mmoja yanaweza kuvuruga matarajio yoyote ya kuanzisha taifa la Palestina na kufikiwa kwa makubaliano ya amani ya mataifa mawili.

Maas alisema kabla ya kuondoka Ujerumani kwamba "watu wengi nchini Israel na hata Umoja wa Ulaya bado wanatilia maanani hatua zilizopigwa katika mchakato wa kusaka amani ya Mashariki ya Kati pamoja na uwezekano wa mipango ya kuyanyakua maeneo hayo.

Waziri Maasi akiwa na waziri wa mambo ya nje wa israel Gabi AshkenaziPicha: picture-alliance/dpa/I. Yefimovich

Alisema Ujerumani bado inasimamia lengo la suluhu ya mataifa mawili na kuongeza kuwa hilo pia watalijadili na watasisitiza kwamba wako tayari kuunga mkono mikakati yote ya kuanzisha tena mazungumzo kati ya Israel na Palestina.

Ujerumani, ambayo tayari ni msuluhishi muhimu miongoni mwa mataifa ya Ulaya, itachukua nafasi ya urais, ambayo huwa ni ya kupokezana kwenye Halmashauri ya Umoja wa Ulaya na rais wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kuanzia mwezi ujao, inaweza kuwa na kauli nzito katika uwezekano wa kuiwekea vikwazo Israel kuhusu mpango wake huo.

Soma Zaidi:EU: Msimamo kuhusu makaazi ya walowezi hautobadilika 

Baada ya kukutana na Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Israel, Gabi Ashkenazi, Maas pia alipangiwa kukutana na Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu na Waziri wa Ulinzi Benny Gantz, baadae leo na hatimaye kwenda nchi jirani ya Jordan kukutana na waziri wa mambo ya nje na kufanya mkutano kwa njia ya simu na viongozi wa Palestina.

Makazi ya walowezi wa Kiyahudi, yaliyoko katika Ukingo wa MagharibiPicha: picture-alliance/AP Photo/M. Illean

Mpango wa Marekani una lengo la kuyaacha angalau theluthi moja ya maeneo ya Ukingo wa Magharibi ambayo Israel iliyanyakua mwaka 1967, chini ya udhibiti kamili ya Israel. Wapalestina wanaotaka eneo lote la Ukingo wa Magharibi kuwa sehemu ya taifa huru wameupinga mpango huo, wakisema unawapendelea pakubwa Israel.

Kujibu hatua hiyo, Palestina ikakata ushirikiano muhimu wa kiulinzi na Israel na kusema hawataendelea kufungwa na makubaliano yaliyosainiwa. Hatua hizo zimeibua wasiwasi wa kurejea kwa machafuko iwapo hatua ya kuyanyakua maeneo hayo itatekelezwa. Waziri wa ulinzi wa Israel, ameliomba jeshi kujiandaa mara moja kukabiliana na kile kinachodhaniwa ni maandamano mabaya ya Wapalestina dhidi ya hatua hiyo.

Soma Zaidi: Kiongozi wa Palestina aondoa makubaliano yake na Israel na Marekani

Pendekezo hilo pia linakabiliwa na upinzani nchini Israel kwenyewe, ingawa Netanyahu ameonekana kudhamiria kutekeleza hatua hiyo kabla hata ya uchaguzi wa Marekani mwezi Novemba. Joe Biden, anayetarajiwa kugombea urais kupitia chama cha Democratic, na ambaye huenda akashinda nafasi hiyo, alikwishaweka wazi kwamba anapinga pendekezo hilo la kunyakua maeneo ya Ukingo wa Magharibi.

Mashirika: APE/AFPE.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW