1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaHaiti

Ghasia za magenge ya wahalifu zaongezeka nchini Haiti

28 Septemba 2023

Umoja wa Mataifa umesema ghasia zinazosababishwa na magenge ya wahalifu zinaongezeka nchini Haiti na zimeenea kwenye miji mingine miwili mikubwa ya Gonaives na Cap-Hatien kutoka kwenye mji mkuu Port-au-Prince.

Haiti Protest gegen Ministerpräsident Ariel Henry
Picha: Odelyn Joseph/AP Photo/picture alliance

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameyasema hayo katika ripoti yake mpya kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Amesema watu wapatao 2,728 wameorodheshwa kuuawa kimakusudi kati ya Oktoba mwaka jana wa 2022 na Juni mwaka huu miongoni mwao wakiwemo wanawake 247, wavulana 58 na wasichana 20.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio GuterresPicha: Mary Altaffer/AP/picture alliance

Magenge hayo ya wahalifu pia yanaendelea kutumia unyanyasaji wa kijinsia ikiwa ni pamoja na ubakaji wa kundi la wahalifu dhidi ya mhanga mmoja kwa lengo la kuwatishia watu walio chini ya udhibiti wa magenge pinzani amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres.

Soma pia:Marekani na Kenya zatia saini makubaliano ya ulinzi kabla ya kuanza mpango wa kupeleka kikosi cha walinda usalama nchini Haiti

Ameelezea matukio 452 za ubakaji yaliorodheshwa katika kipindi cha kuanzia mwezi Oktoba 2022 hadi mwezi Juni 2023. Guterres amesema karibu watu 130,000 wamelazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na ghasia za magenge hayo na hakuna hatua thabiti zilizofikiwa tangu lilipopitishwa azimio la Oktoba mwaka jana.

Amesema Haiti haina mfumo madhubuti wa mahakama unaoweza kushughulikia kesi zinazowakabili wahusika wa magenge hayo ya uhalifu na kwamba nguvu ya magenge hayo ni kubwa kuliko taasisi za kitaifa zilizo dhaifu.

Waziri Mkuu wa Haiti Ariel HenryPicha: Craig Ruttle/AP Photo/picture alliance

Polisi wa Haiti wameshindwa kukabiliana na magenge yenye nguvu licha ya kuongezewa bajeti. Guterres amesema polisi ya Hiti pia inakabiliwa na upungufu wa wafanyakazi kutokana na baadhi yao kujiuzulu wengine wanastaafu na wengine wanauawa wakati wakiwa wanatimiza majukumu yao ya kazi.

Soma pia:Magenge yenye silaha nchini Haiti yataka serikali ipinduliwe

Katibu Mkuu Guterres pia amewasilisha ripoti kuhusu maendeleo katika kulitimiza azimio la Baraza la Usalama lililopitishwa Oktoba mwaka jana juu ya vikwazo dhidi ya kiongozi wa genge moja la wahalifu nchini Haiti.

Rais wa Kenya William RutoPicha: Khalil Senosi/AP/picture alliance

Wakati huo huo wajumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wanalijadili azimio jipya la umoja huo juu ya kuidhinisha kikosi cha kimataifa ambacho hakitakuwa chini ya Umoja wa Mataifa.

Badala yake kitaongozwa na Kenya kwa ajili ya kulinda usalama na kupambana na magenge ya nchini Haiti. Wanadiplomasia wamesema azimio hilo litapigiwa kura baadaye wiki hii au wiki ijayo.

Chanzo: AP

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW