1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN, Marekani zaishinikiza Uganda kuhusu haki za binadamu

13 Januari 2021

Marekani imelaani kufungwa kwa mitandao ya kijamii nchini Uganda kuelekea uchaguzi na katibu mkuu wa UN Antonio Guterres amehimiza kuheshimiwa kwa haki za binadamu. Serikali ya Uganda imekataa kuwathibitisha waangalizi.

Uganda Bobi Wine
Picha: Ronald Kabuubi/AP Photo/picture alliance

Uganda iliamuru kufungwa kwa majukwaa ya mitandao ya kijamii ikiwemo Facebook na WhatsApp kuelekea uchaguzi wa Alhamisi ambamo rais Yoweri Museveni, alieko madarakani tangu 1986, anatafuta muhula wa sita.

"Tuna wasiwasi kuhusu ripoti kwamba serikali ya Uganda imewaamuru watoa huduma za intaneti kuzuwia mitandao ya kijamii, app za kutuma ujumbe na kuchagua maudhui kuelekea uchaguzi," alisema Tibor Nagy, mwanadiplomasia wa juu wa Marekani barani Afrika. "Vikwazo kama hivyo vinadhoofisha haki za binadamu na uhuru wa msingi."

Soma pia: Rais Yoweri Museveni afungia Facebook nchini Uganda

Taarifa hiyo imetolewa katikati mwa utata nchini Marekani kwenyewe, ambako Twitter na Facebook zimefunga kurasa za mitandao ya kijamii ya Rais Donald Trump kwa kuchochea wafuasi wake kuvamia bunge la Marekani kuhusiana na kushindwa kwake katika uchaguzi.

Rais wa sasa Yoweri Museveni anawania muhula wa sita, lakini serikali yake inakosolewa kwa ukiukaji mkubwa wa haki na kukandamiza upinzani.Picha: Hannah McKay/Getty Images

Museveni mwenye umri wa miaka 76, anakabiliana na nyota wa muziki aliegeuka mbunge Robert Kyagulanyi, maarufu Bobi Wine mwenye umri wa miaka 38, ambaye amewahamaisha vijana waliokuwa kwa sehemu kubwa wakimjua rais moja tu.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres "aliwamihimiza wanasiasa wote na wafuasi wao kuendesha shughuli zao za kisiasa kwa njia amani na kujizuwia kuchochea vurugu au matamshi ya chuki," msemaji wake Stephane Dujarric alisema.

"Tumeshuhudia kamatakamata na kufungwa kwa wagombea," Dujarric alisema. Kampeni za uchaguzi huu zimekuwa moja ya zilizokumbwa na umwagaji damu mkubwa katika kipindi cha miaka kadhaa.

Waandishi habari wanaoripoti mikutano ya kampeni wameshambuliwa, wakosoaji wa serikali kufungwa na wasimamizi wa uchaguzi wameshtakiwa, na kuzusha hofu juu ya uwazi wa mchakato wa uchaguzi huo. Maandamano ya siku mbili mwezi Novemba yalisababisha vifo vya watu 54.

Soma pia: Je uchaguzi utakuwa wa huru na haki Uganda?

Waangalizi wa Marekani wanyimwa vibali

Balozi wa Marekani nchini Uganda alisema ubalozi umefuta mipango ya kuweka waangalizi katika uchaguzi, akitoa sababu ya uamuzi wa maafisa wa uchaguzi kuwanyika idhini wanachama wengi zaidi wa timu ya waangalizi wa Kimarekani.

Mgombea mkuu wa upinzani, Robert Kyagulanyi aka Bobi Wine ambaye amempa wakati mgumu Museveni katika kampeni za mwaka huu.Picha: Nicholas Bamulanzeki/AP/picture alliance

Balozi Natalie E. Brown alielezea kusikitishwa kwake katika taarifa akisema zaidi ya asilimia 75 ya maombi ya waangalizi yalikataliwa. "Kwa asilimia 15 tu ya maombi yalioidhinishwa, haiwezikani kwa Marekani kufanya uangalizi wa maana kwenye vituo vyote nchini," ilisema taarifa hiyo.

"Kama tulivyofahamisha huko nyuma, Marekani haiegemei upande woowte katika uchaguzi ujao nchini Uganda. Tunaunga mkono mchakato wa uchaguzi ulio huru na wa haki, wa amani na shirikishi."

Bila ushiriki mpana wa waangalizi," aliongeza taarifa hiyo, uchaguzi wa Uganda utakosa uwajibikaji, uwazi na imani ambavyo ujumbe wa waangalizi unatoa." Msemaji wa tume ya uchaguzi hakupatikana mara moja kuzungumzia suala hilo.

Chanzo: Mashirika.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW