1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroAfrika

UN: Rwanda inao udhibiti na mamlaka kwa M23

2 Julai 2025

Ripoti ya siri iliyotolewa na kundi la wataalamu wa Umoja wa Mataifa inasema Rwanda ilikuwa na udhibiti na mamlaka kwa waasi wa M23 wakati wa operesheni zao mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Goma 2025 | Wapiganaji wa kundi la waasi wa M23 wakiwa mashariki mwa DRC
Wapiganaji wa kundi la waasi wa M23 mjini Goma, mashariki mwa DRCPicha: Arlette Bashizi/REUTERS

Ripoti hiyo iliyofichuliwa na shirika la habari la Reuters inaelezea msaada wa kijeshi ambao Rwanda iliutoa kwa wapiganaji wa M23 ikiwa ni pamoja na mafunzo na vifaa vya kiteknolojia vya hali ya juu vilivyokuwa na uwezo wa kuvuruga mifumo ya ulinzi wa anga wa jeshi la Kongo lililokuwa limeelemewa, jambo ambalo liliwapiga jeki waasi hao.

Wataalam hao wanasema hatua hiyo iliiwezesha Rwanda kuwa na ushawishi wa kisiasa na kuweza kulifikia eneo la  mashariki mwa DRC  lenye utajiri wa madini na lililokumbwa na mizozo kwa zaidi ya miongo mitatu.

Aidha ripoti hiyo imeendelea kubainisha kuwa Rwanda iliwapokea viongozi wa muungano wa waasi unaojumuisha M23 katika vituo vyake vya Gabiro, Nasho na Gako ambako wapiganaji wa M23 walipewa mafunzo ya kijeshi. Pia, wataalam hao wanasema Rwanda iliongeza idadi ya wanajeshi wake hadi kufikia 6,000 katika majimbo ya Kivu Kaskazini na Kusini.

Maafisa wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa MONUSCO nchini DRCPicha: Alexis Huguet/Getty Images/AFP

Wanadiplomasia wameeleza kuwa ripoti hiyo inayotarajiwa kuchapishwa hivi karibuni, iliwasilishwa mapema mwezi Mei kwa kamati ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa inayofuatilia mzozo wa  Kongo  na inayo husika pia na kuweka vikwazo.

Mwezi Januari na Februari, waasi wa M23 walipata mafanikio makubwa mashariki mwa Kongo kwa kuchukua udhibiti wa miji mikubwa zaidi eneo hilo ya Goma na Bukavu.

Rwanda yatajwa kuhusika moja kwa moja

Kwa muda kadhaa sasa,  Kongo, Umoja wa Mataifa na nchi za Magharibi wamekuwa wakieleza bayana kwamba Rwanda inaiunga mkono M23 kwa kuipatia askari na hata silaha.

Hata hivyo serikali mjini Kigali imekuwa ikikanusha tuhuma hizo ikidai kuwa vikosi vyake vimekuwa vikijilinda dhidi ya jeshi la Kongo na wanamgambo wa kihutu wa FDLR  ambao wanaohusishwa na mauaji ya kimbari dhidi ya watutsi ya mwaka 1994 huko Rwanda.

Rais wa DRC Felix TshisekediPicha: DW

Lakini ripoti hii iliyotolewa na wataalamu wa Umoja wa Mataifa inakanusha madai hayo na kusema kuwa msaada wa jeshi la Rwanda kwa M23 haukulenga kimsingi kushughulikia vitisho vinavyotolewa na FDLR, na kwamba Kigali ililenga "kujinyakulia maeneo zaidi" huko mashariki mwa Kongo.

Mpaka sasa, ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Rwanda na hata wasemaji wa serikali za Kongo na Rwanda hawajazungumza chochote juu ya ripoti hiyo. Ikumbukwe kuwa mnamo Juni 27, chini ya upatanishi wa Marekani, Rwanda na Kongo zilisaini makubaliano ya amani  mjini Washington.

Mkataba huo hata hivyo umekosolewa na baadhi ya watu wakiutaja kama makubaliano ya kibiashara yatakayozinufaisha nchi za Magharibi kwa mabilioni ya dola hasa kutokana na uwekezaji wao katika eneo hilo tajiri lenye madini mbalimbali ikiwa ni pamoja na tantalum, dhahabu, cobalt, shaba na lithium. Lakini viongozi wa Kinshasa wanadai kuwa watalinda maslahi ya nchi yao.

(Chanzo: Reuters)

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW