1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSyria

UN yamuondolea vikwazo Rais Sharaa wa Syria

7 Novemba 2025

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limemuondolea vikwazo Rais wa Syria Ahmed al-Sharaa anayetarajiwa kukutana na Rais Donald Trump wa Marekani Jumatatu ijayo.

Marekani New York 2025 | Rais wa Syria Ahmed al-Sharaa
Rais Mpya wa Syria Ahmad Al-Sharaa alipohudhuria sherehe ya kuadhimisha ushindi wa mapinduzi ya Syria huko Aleppo, Syria Mei 27, 2025.Picha: Bashir Daher/IMAGO

Azimio hilo lililoandaliwa na Marekani na kupitishwa jana Alhamisi pia limemuondolea vikwazo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Syria Anas Khattab. Liliidhinishwa kwa kura 14, lakini China ilijizuia.

Washington imekuwa ikiwarai wanachama 15 wa baraza hilo kuilegezea Syria vikwazo. Na mnamo mwezi Mei, Rais Donald Trump alitangaza mabadiliko makubwa ya kisera kuelekea taifa hilo, aliposema ataiondolea vikwazo.

Baada ya kuidhinishwa, Trump alimsifu Sharaa kwa kufanya kazi nzuri na hatua kubwa imepigwa nchini humo licha ya mazingira magumu.

"Tutakutana... Na nadhani anafanya kazi nzuri sana. Ni mazingira magumu Na yeye ni mtu mahiri. Lakini ninaelewana naye vizuri sana, na hatua kubwa imepigwa kuhusu Syria. Hilo ni jambo gumu, lakini hatua kubwa imepigwa. Tuliondoa vikwazo kwa ombi la Uturuki na Israel," Trump aliwaambia waandishi wa habari.

HTS iliwekewa vikwazo tangu 2014

Baada ya miaka 13 ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, Rais Bashar al-Assad alifurushwa mnamo mwezi Disemba kufuatia mashambulizi yaliyofanywa na vikosi vilivyoasi vikiongozwa na kundi la Islamist Hayat Tahrir al-Sham (HTS).

Assad akimbia nchi, waasi waukamata Damascus

01:45

This browser does not support the video element.

Kundi hilo ambalo awali lilitambulika kama Nusra Front, lilikuwa ni tawi rasmi la kijeshi la kundi la kigaidi la al Qaeda nchini Syria hadi pale lilipovunja uhusiano mwaka 2016. Tangu Mei, 2014, kundi hilo lilikuwa chini ya vikwazo vya Umoja wa Mataifa vilivyolenga makundi ya al Qaeda na lile linalojiita Dola la Kiislamu, IS.

Wafuasi wengi wa HTS pia wanakabiliwa na vikwazo hivyo, kuanzia kuzuiwa kusafiri, mali zao kuzuiwa hadi vizuizi vya silaha. Lakini sasa Sharaa na Khattab wako huru.

China yalipinga azimio la UN

Hata hivyo China ilijizuia kupiga kura kwa kuwa ilisema azimio hilo halikuelezea kwa kina juu ya namna suala la ugaidi litakavyoshughulikiwa pamoja na hali ya usalama nchini Syria, hii ikiwa ni kulingana na Balozi wa China kwenye Umoja wa Mataifa Fu Cong.

Gereza Nambari 3 iliyoko Dabancheng katika Mkoa Unaojiendesha wa Xinjiang Uyghur magharibi mwa China mnamo Aprili 23, 2021. Makundi ya haki za binadamu na mataifa ya Magharibi yakiongozwa na Marekani, Uingereza na Ujerumani yaliishutumu China kwa kuikandamiza jamii ya wachache ya UyghurPicha: Mark Schiefelbein/AP Photo/picture alliance

China kwa muda mrefu imekuwa ikielezea wasiwasi wake kuhusiana na mustakabali wa Vuguvugu la itikadi kali la Eastern Turkistan Islamic Movement (ETIM) huko nchini Syria, ambalo wanamgambo wa Uyghur kutoka China na Asia ya Kati ni wafuasi wake. Na makundi ya haki za binaadamu yamekuwa yakiishutumu Beijing kwa kuinyanyasa jamii hiyo ya walio wachache.

Hata hivyo Fu amesema azimio hilo limeweka wazi kwamba Syria inapaswa "kuchukua hatua madhubuti za kupambana na vitendo vya kigaidi" na kushughulikia kitisho cha wanamgambo wa kigeni wa makundi ya kigaidi, ambayo ni pamoja na vuguvugu hilo la ETIM lililoko nchini Syria.

Balozi wa Urusi kwenye Umoja huo Vassily Nebenzia kwa upande wake amesema Moscow inaunga mkono azimio hilo kwa sababu ya umuhimu wake na imetanguliza maslahi na matarajio ya watu wa Syria.

Urusi ilimlinda kidiplomasia mshirika wake Assad wakati wa vita, ikipiga kura ya turufu zaidi ya mara kumi na mbili katika Baraza la Usalama, mara nyingi ikiungwa mkono na China wakati Baraza hilo lilipokutana mara kadhaa kujadili hali ya kisiasa na kibinadamu nchini Syria

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW