1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya Kursk yadhihirisha udhaifu wa Urusi?

Angela Mdungu
22 Agosti 2024

Saa kadhaa kabla ya wanajeshi wa Ukraine kufanya uvamizi katika mpaka magharibi mwa Urusi, hakukuwa na kiashiria chochote cha kuwepo kwa tatizo ndani ya Urusi.

Mkaazi akiwa kasimama nje ya nyumba yake ilioharibiwa kwa mashambulizi ya Urusi na Ukraine.
Mkaazi wa Urusi akiwa amesimama nje ya nyumba yake ilioharibiwa baada ya mashambulizi ya majibizano kati ya Urusi na Ukraine.Picha: Alexander Ermochenko/REUTERS

Usiku wa manane kuamkia Agosti 6, Wizara ya Ulinzi ya Urusi ilichapisha habari njema  kwamba, zaidi ya wanajeshi 2,500 waliofanikisha kuuteka mji mmoja mashariki mwa Ukraine wangepewa nishani za taifa za ushujaa. Hata hivyo, ndani ya nchi hiyo mambo yalikuwa tofauti. 

Asubuhi ya Agosti sita, wakati Ukraine ilipokuwa ikifanya moja kati ya uvamizi mkubwa zaidi ndani ya Urusi tangu Vita vya Pili vya Dunia, Wizara ya Ulinzi ilichapicha video iliyomuonesha Mkuu wa utumishi wa jeshi la Urusi Jenerali Valery Gerasimov, akiyatembelea maeneo tofauti ya uwanja wa mapambano ikiwemo ndani ya Ukraine. 

Alipokea taarifa za mwenendo wa hali kutoka kwa makamanda wa jeshi na kuainisha kazi kwa ajili ya hatua nyingine zinazofuata. Video hiyo haikuonesha muda hasa wa ziara yake.

Soma pia:Putin aishtumu Ukraine kujaribu kukishambulia kinu cha nyuklia

Haikuonesha wasiwasi wowote au taarifa kuhusu matukio yaliyokuwa yakiendelea katika mkoa wa Kursk yaliyomkasirisha na kutibua mipango yake.

Hofu ilienea haraka miongoni mwa wakaazi wa eneo hilo la magharibi mwa Urusi katika saa za awali za uvamizi huo licha ya majaribio kadhaa ya mamlaka ya kuwahakikishia kuwa kila kitu kilikuwa sawa.

Ukreine kufanya mashambulizi ya kimkakati

Uwezekano wa kuwa Ukraine ingeweza kubadili hali ya mambo na kuivamia Urusi haukudhaniwa kabla ya uthubutu huo. Operesheni hiyo ya ghafla imibua maswali kuhusu ufanisi wa ulinzi wa Urusi, uthabiti wa mipaka na ubora wa vikosi vinavyoilinda.

Mtafiti wa masuala ya jeshi wa Ufaransa Yohann Michel katika mahojiano ya hivi karibuni alisema kuwa, Urusi ilifeli kabisa kwenye suala la intelijensia kuhusu uvamizi huo.

Kituo cha ukaguzi cha Urusi kikiwa kimeshambuliwa na Ukraine katika oparesheni huko Kursk.Picha: Chubotin Kirill/Ukrinform/ABACA/IMAGO

Viongozi wa Urusi walikaa kimya baada ya tukio hilo hadi Agosti 07, ambapo Rais Vladimir Putin na Jenerali Gerasimov, walipojitokeza na kutoa maoni kwa mara ya kwanza hadharani  kuhusu uvamizi huo.

"Utawala wa Kyiv umefanya uchokozi mwingine wa kiwango kikubwa. Unafanya mashambulizi bila kujali kwa kutumia silaha za aina mbalimbali yakiwemo makombora dhidi ya miundombinu ya raia, makaazi ya watu na magari ya wagonjwa."

Jenerali Gerasimov, alimwambia Rais Putin mbele ya televisheni kuwa wanajeshi wa Urusi walifanikiwa kuwazuia wapiganaji wa Ukraine wasisonge mbele zaidi mkoani Kursk.

Soma pia:Vita vya Ukraine vyatawala kampeni za majimbo Ujerumani

Mchambuzi Yohan Michel anasema haifahamiki ikiwa Jenerali huyo alipewa taarifa za kupotosha na wasaidizi wake au kama alilazimika kumpa Putin habari njema mbele ya kamera,  katika kile mchambuzi huyo alichokiita kuwa ni  "kumpa mkubwa wa kazi kile anachotaka kusikia au kukiona mbele ya umma katika wakati maalumu"

Wakati vikosi vya Ukraine vikirudi nyuma mashariki mwa Ukraine, huenda Moscow ilidhani kwamba Kyiv isingechukua hatua hiyo hatari ambayo hadi sasa haifahamiki wazi kama itakuwa manufaa ama la.

Malengo ya Ukraine Kursk

Madhumuni ya Ukraine katika mkoa wa Kursk ni pamoja na kuwavuruga wanajeshi wa Urusi walio katika mapambano kwenye mkoa wa mashariki mwa Ukraine wa Donetsk.

Badala yake, mapigano yamepamba moto katika mkoa huo katika siku za hivi karibuni huku hatari zikizidi kuongezeka kwa Ukraine wakati ikijitahidi kuendeleza udhibiti wake katika mkoa wa Kursk.

Siku mbili baada ya vikosi vya Ukraine kuingia Urusi, mbunge na afisa wa zamani wa jeshi la Urusi Andrei Gurulyov, alisema katika mahojiano ya televisheni kuwa, viongozi wa jeshi nchini humo walishapewa angalizo katika taarifa iliyotolewa mwezi mmoja kabla, juu ya kuwepo kwa ishara za shambulio kutoka Kyiv. Hata hivyo, hawakutilia maanani ripoti hiyo.

Soma pia:Rais Putin afanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa China Li

Wizara ya Ulinzi ya Urusi ilipotafutwa ili ijibu kuhusu hilo, haikujibu. Nalo jeshi la Urusi lilikataa kuzungumzia kuhusu operesheni inayoendelea.

Mashambulizi ya Urusi yameua zaidi ya watu 30 Ukraine

02:10

This browser does not support the video element.

Hata Wizara ya mambo ya kigeni ya Marekani, wizara ya Ulinzi na ikulu ya Marekani ya White House hazikupatikana kutoa ufafanuzi.

 

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW