1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Urusi: Mashambulio ya droni kuilenga Moscow hayakufanikiwa

21 Agosti 2024

Mamlaka ya Urusi imesema mashambulio ya droni kutoka Ukraine yaliyoulenga mji wa Moscow hayakufanikiwa. Urusi imesema hayo ni mashambulio makubwa kabisa tangu vita vilipoanza mnamo mwaka 2022

Russland Porträt Wladimir Putin
Picha: Vyacheslav Prokofyev/picture alliance

Wizara ya ulinzi ya Urusi imeeleza kuwa mfumo wake wa ulinzi wa anga uliharibu droni 11 katika mji mkuu Moscow na maeneo yaliyo karibu na jiji hilo.

Meya wa jiji la Moscow Sergei Sobyanin, amesema hili ni moja kati ya majaribio makubwa kuwahi kutokea la kutaka kuushambulia mji wa Moscow kwa kutumia ndege zisizo na rubani. Meya huyo amesema katika mashambulio hayo ya usiku wa kuamkia leo hakuna uharibifu au hasara yoyote iliyotokea.

Picha inayoonesha daraja lililopigwa na majeshi ya Ukraine katika eneo la Kursk upande wa UrusiPicha: Ukrainian Armed Forces/AP/picture alliance

Majaribio ya Ukraine ya hivi karibuni ya kuulenga mji mkuu wa Urusi, Moscow ni makubwa kuliko mashambulio ya mwezi Mei mwaka jana.

Soma Pia: Ukraine, Urusi zadai kuimarisha mashambulizi  

Mashambulizi hayo ya droni yanafanyika huku vikosi vya Ukraine vikiendelea kupambana katika eneo la Kursk Magharibi mwa Urusi.

Idara ya sera ya Taasisi inayofanya utafiti wa vita, iliyoko Washington, Marekani imesema katika ripoti yake ya kila siku kwamba jeshi la Ukraine limepiga hatua na kupata ufanisi wa ziada katika operesheni yake ya sasa, ambayo imeingia katika wiki yake ya tatu.

Taasisi hiyo imebainisha kuwa vikosi vya Ukraine vimefaulu kuyalipua madaraja na vifaa vya uhandisi vya Urusi kwenye Mto Seym katika eneo la magharibi mwa mkoa wa Kursk na kwamba mafaniko hayo yameongeza ujasiri na ari nchini Ukraine kwamba sasa nchi hiyo imefaulu kuubadilisha muelekeo wa mapigano kati yake na Urusi.

Soma Pia: Urusi na Ukraine zaendelea kupambana vikali huko Kursk  

Lakini taasisi hiyo imekumbusha kuwa wakati Ukraine inafurahia ushindi wa upande mmoja nchi hiyo inaendelea kupoteza ardhi katika kanda yake ya mashariki iliyo na viwanda.

Naibu mkuu wa Baraza la Usalama la Urusi, Dmitry MedvedevPicha: Alexander Astafyev/Russian Government/Tass/IMAGO

Naibu mkuu wa baraza la usalama la Urusi, Dmitry Medvedev, amesema leo Jumatano kwamba uvamizi wa Ukraine katika eneo la Kursk ndani ya ardhi ya Urusi unamaanisha kuwa mazungumzo ya kuvimaliza vita kati ya Moscow na Kyiv hayatakuwepo hadi Urusi itakapoishinda Ukraine ikwenye uwanja wa vita.

Kwa upande wake kiongozi wa Chechnya Ramzan Kadyrov alipokutana na Rais wa Urusi Vladimir Putin anayefanya ziara yake ya kwanza katika eneo hilo tangu mwaka 2011 kwamba  eneo lake limepeleka wapiganaji zaidi 47,000 katika eneo la mzozo kati ya Urusi na Ukraine.

Soma Pia: Urusi bado yapambana na wanajeshi wa Ukraine waliovuka mpaka  

Naye Sergei Chemezov, mshirika wa karibu wa Rais wa Urusi Vladimir Putin, amesema kuna hatari kubwa ya kusababisha vita vitakavyozagaa duniani iwapo Marekani na washirika wake wa Magharibi wataendelea kuchochea migogoro nchini Ukraine na kuruhusu majeshi ya Ukraine kushambulia ndani ya Urusi.

Vyanzo: RTRE/AP

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW