1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi yaikabidhi Ukraine miili ya wanajeshi waliouawa vitani

Amina Abubakar afp,reuters
9 Aprili 2026

Urusi hii leo imeikabidhi Ukraine miili ya wanajeshi wake1000 huku Kyiv nayo ikirejesha miili ya wanajeshi 41 wa Urusi, waliouwawa katika vita vya pande hizo mbili, vilivyoingia mwaka wake wa nne.

Belarusisch-ukrainische Grenze 2025 | Austausch der Leichen von getöteten ukrainischen und russischen Soldaten
Urusi yaikabidhi Ukraine miili 1,000 ya wanajeshi wake waliouwawa vitaniPicha: Official Telegram channel of top Russian negotiator and Kremlin aide Vladimir Medinsky @vr_medinskiy/AFP

Mara kwa mara pande hizo  mbili hasimu zimekuwa zikibadilishana miili ya wanajeshi waliouwawa vitani, ikiwa ni sehemu ya makubaliano madogo katika mgogoro huo unaoendelea na uliosababisha mauaji ya maelfu ya watu tangu ulipoanza Februari 24 mwaka 2022.

Video ya shirika la Ruptly linalomilikiwa na serikali ilionyesha wanaume waliokuwa wamevalia nguo za buluu na glavu nyeupe, wakibeba mifuko mikubwa meupe ya kuhifadhia maiti ikihamishwa kutoka kwenye gari moja hadi jengine. Miili hiyo inadaiwa kuhamishwa chini ya uangalizi wa Shirika la Msalaba Mwekundu. 

Makao makuu ya uratibu wa hali ya wafungwa wa kivita ilithibitisha kupitia mtandao wake wa kijamii kwamba miili 1000 waliopokea ilikuwa ni wa wanajeshi wa Ukraine. Kyiv imewahi kuituhumu Moscow kukabidhi miili ya wanajeshi wa Urusi waliouawa vitani ikidai ni wanajeshi wa Ukraine. Ukraine imesema baada ya miili hiyo kutambuliwa itapelekwa kwa familia zao kwa maziko.

Urusi yaikabidhi Ukraine miili 1,000 ya wanajeshi wake waliouwawa vitaniPicha: Official Telegram channel of top Russian negotiator and Kremlin aide Vladimir Medinsky @vr_medinskiy/AFP

Vita hivyo vya Urusi na Ukraine, viliuanzisha mgogoro mbaya  kuwahi kushuhudiwa barani Ulaya tangu Vita vya Pili vya Dunia, huku mamilioni ya watu wakipoteza makaazi yao, pamoja na mauaji ya maelfu ya raia yakiripotiwa katika pande zote mbili. 

Manowari za Urusi zazuiwa kufanya operesheni ya 'uhalifu'

Kwengineko Uingereza na Norway na mataifa mengine yalishiriki operesheni ya wiki nzima, kuzuwia manowari za kijasusi za Urusi  kufikia nyaya za chini ya maji katika eneo la kaskazini mwa eneo la Atlantiki, zikiishutumu Urusi kutumia vita vya Iran kupanga shughuli za uchochezi dhidi ya Ulaya. 

Kulingana na Waziri wa Ulinzi wa Uingereza John Healey, operesheni hiyo ilihusisha meli ya kivita ya Jeshi la Wanamaji la Uingereza, ndege na mamia ya wanajeshi, na ilifanikiwa kuzuia manowari za Urusi kufanya shughuli alizozitaja kuwa za kihalifu. 

Waziri wa Ulinzi wa Uingereza John HealeyPicha: Christian Mang/REUTERS

Aliongeza kuwa vyombo hivyo vya Urusi hatimaye viliondoka baada ya operesheni iliyodumu zaidi ya mwezi mmoja. Mataifa ya NATO yamekuwa yakionya mara kwa mara kuhusu hatari ya Urusi kuhujumu nyaya za mawasiliano ya kimataifa chini ya bahari, madai ambayo Moscow imekuwa ikiyakanusha.

Kundi la Memorial laidhinishwa kama kundi la kigaidi

Huku hayo yakiarifiwa Mahakama ya juu ya Urusi imeliweka katika orodha ya wahalifu kundi la kutetea haki za binaadamu la Memorial lililowahi kutunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel, Hatua hiyo ni sehemu ya kamata kamata inayoendelea dhidi ya wapinzani na mashirika ya kiraia nchini humo huku huku vita vya taifa hilo na Ukraine vikiendelea kushika kasi.

Mahakama ya juu ya Urusi imeliweka katika orodha ya wahalifu kundi la kutetea haki za binaadamu la Memorial lililowahi kutunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel.Picha: NATALIA KOLESNIKOVA/AFP/Getty Images

Kufuatia shauri la faragha lililosikilizwa hii leo mahakama hiyo ilitoa uamuzi huo kulingana na ombi la wizara ya sheria iliyotaka shirika hilo kuidhinishwa kama kundi la kigaidi huku shughuli zake zikipigwa marufuku nchini Urusi. 

Awali kundi hilo la Memorial lilipinga madai hayo lakini uamuzi uliotolewa unaipa nguvu mamlaka kudhibiti miradi yoyote ya kundi hilo pamoja na wafuasi wake. Shirika hilo ni moja ya shirika kongwe na mashuhuri linalotetea haki za binaadamu Urusi na lilikabidhiwa tuzo ya amani ya nobel ya mwaka 2022 ikiwa ni chini ya mwaka mmoja tangu uvamizi wa Urusi ulipoanzishwa dhidi ya Ukraine. 

Kamati ya Nobel imeukosoa uamuzi huo ikisema ni ukiukaji wa maadili ya utu na uhuru wa kujieleza huku ikiitolea mwito Urusi kuacha mara moja unyanyasaji wa kundi hilo na wanachama wake. 
 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW