1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi yashambulia kinu cha Nyuklia cha Ulaya

Hawa Bihoga
4 Machi 2022

Vikosi vya Urusi vimekishambulia kinu kikubwa zaidi cha nyuklia barani Ulaya kilichopo kusini mashariki mwa Ukraine baada ya mapigano makali na wanajeshi wa Ukraine, ambayo yalisababisha moto mkubwa na kuzusha hofu.

Ukraine Atomkraftwerk Saporischschja unter Beschuss
Picha: Zaporizhzhya NPP/REUTERS

Idara ya Ukaguzi wa Udhibiti wa Nyuklia ya Ukraine ilisema katika taarifa yao kwamba, eneo la NPP la Zaporizhzhia limetekwa na vikosi vya kijeshi vya Shirikisho la Urusi, taarifa hiyo imeongeza kwamba moto huo ulidhibitiwa na vitengo vya dharura. Hata hivyo, taarifa kuhusu waliofariki na kujiruhiwa hazikutolewa.

Hapo awali, mapigano yaliyozuka kati ya vikosi vya uvamizi vya Urusi na wapiganaji wa Ukraine yalikuwa yakisonga mbele kuelekea mji wa Zaporizhzhia ambayo yalisababisha moto katika kinu hicho, kilichopo kusini mwa Ukraine na ambacho  uzalisha humusi moja ya umeme wa Ukraine.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky aliishutumu Urusi kwa kutumia ugaidi wa nyuklia na kuwasihi viongozi wa dunia waiunge mkono Kyiv.

Soma Pia:Mtambo wa nishati ya nyuklia washambuliwa Ukraine

Katika ujumbe wa video uliotelewa Rais Zelensky alisema hakuna nchi nyingine ispokuwa Urusi ambayo ilikilenga kinu hicho cha nyuklia.

"Watu wa Ulaya, tafadhali amkeni. Waambieni wanasiasa wenu - Wanajeshi wa Urusi wanashambulia mtambo wa nyuklia Ukraine.Alisema Rais Zelensky katika video yake.

Moto wowote karibu na mtambo wa nyuklia unarejesha kumbukumbu ya janga la Chernobyl la mwaka 1986, nchini Ukraine, ambalo lilisababisha vifo vya mamia ya watu na kusambaza uchafuzi wa miale kote barani Ulaya.

"Mtambo wa nyuklia wa Zaporizhzhia. mjini Enerhodar. Kuna vinu sita vya nyuklia huko - sita! Chernobyl ilikuwa mtambo mmoja ambao ulilipuka. Moja tu." Alisisitiza katika video yake.

Sima pia:Urusi yazidisha mashambulizi katika miji ya Ukraine

Urusi:yapitisha muswada kudhibiti taarifa za uongo

Wakati hayo ya kiendelea huko Ukraine, bunge la Urusi limepitisha muswada wa kuwasilisha kifungo cha hadi miaka 15 jela kwa kueneza kwa makusudi kile walichokiita habari za uongo kuhusu hatua za jeshi lake dhidi ya Ukraine.

Muswada huo unatangazwa huku kukiwa kunashuhudiwa ukandamizaji wa mamlaka ya Urusi dhidi ya vyombo vya habari huru na ukosoaji wa uvamizi wa Ukraine wiki iliyopita.

Waandmanaji wakichukizwa na hatua za Putin dhidi ya UkrainePicha: Daniel Reinhardt/dpa/picture alliance

Kwa sasa muswada huo unaelekea kwenye baraza la juu la Bunge, ambalo litaidhinisha rasmi na kuwasilishwa mbele ya Rais Vladimir Putinkwa ajili ya utiaji saini kuwa sheria.

Chini ya saa mbili baada ya muswada huo kupitishwa, tovuti ya habari ya Znak ilisema itasitisha kufanya kazi, ikitaja msururu wa vikwazo ambavyo vimeonekana kuathiri kazi ya vyombo vya habari hivi karibuni nchini Urusi.

Soma Pia:Wanajeshi 70 wa Ukraine wauwawa

Wakati hayo yakijiri Urusi na Ukraine zimekubaliana kuweka njia za kiutu kwa ajili ya raia wanaokimbia mapigano yanayoongezeka, huku Rais Putin akisema kampeni yake inakwenda kama ilivyopangwa na kwa wakati.

Pande hizo mbili zilikutana baada ya vikosi vya Urusi kufanikiwa kuuteka kikamilifu mji wa kwanza mkubwa wa Ukraine, huku Putin akionyesha kutokuwa tayari kusikiliza miito ya kimataifa ya kusitisha uhasama wakati vita hiyo ikiingia katika wiki yake ya pili.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW