Urusi yashambulia Odesa na kuwauwa watu 2
11 Aprili 2026
Watu wengine wawili walijeruhiwa katika shambulio hilo wakati droni hizo zilipolenga eneo la makazi, na kuharibu majengo ya ghorofa, nyumba na shule ya chekechea.
Kwa mujibu wa jeshi la wanahewa la Ukraine, Urusi iliilenga Ukraine kwa droni 160 ambapo 133 zilidunguliwa au kunaswa, saa chache kabla ya kuanza kutekelezwa kwa pendekezo la usitishaji vita kwa sherehe ya Pasaka ya Kiorthodoksi.
Wizara ya Ulinzi ya Urusi pia imesema droni 99 zilizorushwa usiku kucha na Ukraine zilidunguliwa kote nchini Urusi na katika eneo la Crimea inayolikalia.
Siku ya Alhamisi, Rais wa Urusi Vladimir Putin alitangaza kusitisha mapigano kwa masaa 32 mnamo wikendi hii ya Pasaka ya Kiorthodoksi, na kuamuru vikosi vya Urusi kusitisha mapigano kuanzia saa 4 asubuhi ya leo Jumamosi hadi mwisho wa kesho Jumapili.