UU kuzingatia vikwazo vya silaha dhidi ya Uchina
13 Desemba 2003Matangazo
BRUSSELS: UU unataka kuzingatia tena vile vikwazo vyake vya silaha dhidi ya Uchina. Mwenye Kiti wa Baraza la UU, Waziri Mkuu wa Uitalia, Silvio Berlusconi alisema katika mkutano wa kilele wa UU mjini Brussels kwamba katika kulizingatia swali la kuondolewa vikwazo lazima lichunguzwe pia swali la haki za binadamu nchini Uchina. Nchi kadha zimeikwisha onya kwamba usichukuliwe uamuzi wa haraka kwa sababu Uchina inaendelea kukiuka haki za binadamu. Naye Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Joshka Fischer alilaumu kuwa Uchina inaendelea kukiuka haki za binadamu. UU uliamua kuiwekea Uchina vikwazo vya silaha hapo mwaka 1989 baada ya uongozi mjini Beijing kusababisha umwagaji damu mkubwa katika kuvunja maandamano ya kudai demokrasia yaliyofanywa na wanafunzi na wapinzani wa serikali katika mji mkuu wa Uchina, Beijing.