1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vikosi vya Ukraine vyauzuwia msafara wa Urusi kuvuka mto

13 Mei 2022

Vikosi vya Ukraine vimesema kuwa vimeharibu daraja la pantoni na sehemu ya msafara wa magari ya kivita ya Urusi wakati msafara huo ukijaribu kuvuka mto katika mkoa wa Donbas. Ukraine pia imeharibu meli ya Urusi.

Ukraine | Andriy Nebytov
Picha: Ppress service of the Kyiv region police

Urusi imekumbana na vizuwizi kwenye medani ya vita huku Ukraine ikiwafurusha wanajeshi wake kutoka maeneo yalio karibu na mji wa pili kwa ukubwa wa Kharkiv, katika usongaji mbele wa kasi zaidi tangu kuvilazimisha vikosi vya Kremlin kuondoka Kyiv na kaskazini mashariki zaidi ya mwezi mmoja uliopita.

Soma pia: Idadi ya waliokimbia Ukraine yavuka watu milioni 6

Waandishi wa habari wa Reuters wamethibitisha kuwa Ukraine sasa inadhibiti eneo linaloenea hadi ukingo wa Mto Siverskiy Donets, umbali wa karibu kilomita 40 mashariki mwa Kharkiv.

Mwanajeshi wa Ukraine akitembea karibu na kifaru cha kivita cha Urusi kilichoharibiwa, wakati mashambulizi ya Urusi dhidi ya Ukraine yakiendelea, karibu na vijiji vya Staryi katika mkoa wa Kharkiv, Mei 9, 2022.Picha: Vitalii Hnidyi/REUTERS

Ukanda wa video uliotolewa na kamandi ya kikosi cha anga cha Ukraine ulionekana kuonyesha magari kadhaa ya kijeshi yaliyoteketezwa na sehemu za daraja zilizozama kwa kiasi katika mto huo.

Picha hizo zilionyesha magari mengi zaidi yaliyoharibika au kutelekezwa, vikiwemo vifaru, yakiwa msituni na kwenye njia inayoelekea mtoni.

Soma pia: Umoja wa Mataifa kuamua juu ya uchunguzi Ukraine

Ikitoa taarifa za kijasusi za kila siku ya Ijumaa, wizara ya ulinzi ya Uingereza imesema picha hizo zinaonyesha kuwa Urusi imepoteza alau kundi moja la kikosi cha mbinu za kijeshi na vifaa vya daraja la pantoni viliharibiwa wakati wa kuvuka mto Siverskyi Donets magharibi mwa Severodonetsk.

Wizara ya ulinzi ya Uingereza ilisema Urusi inawekeza juhudi kubwa za kijeshi kusini zaidi kutoka Kharkiv, karibu Izium na Severodonetsk, na ilikuwa ikijaribu kuvunja vizuwizi kuelekea Sloviansk na Kramatorsk.

Miito ya kuokolewa wapiganaji Azovstal

Wapiganaji wa kikosi maalumu cha Azov cha jeshi la ulinzi wa Ukraine waliojeruhiwa katika mapigano dhidi ya vikosi vya Urusi wakiwa ndani ya kiwanda cha chuma cha Azovstal mjini Mariupol, Ukraine, Mei 10, 2022.Picha: Dmytro 'Orest' Kozatskyi/ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Katika mji mkuu wa Kyiv, wake na jamaa za wapiganaji wa Ukraine waliojichimbia kwenye kiwanda cha chuma cha Azovstal katika bandari ya kusini ya Mariupol waliandamana kudai kuokolewa kwa jamaa zao.

Vikosi vya Urusi vimekuwa vikishambulia kiwanda hicho, ambacho ndiyo ngome ya mwisho ya kikosi kinachojiita watetezi wa Ukraine katika mji unaotawaliwa kabisa na Urusi baada ya kuzingirwa kwa zaidi ya miezi miwili.

Soma pia: EU na Japan kuzidisha mbinyo dhidi ya Urusi

"Nawataka watetezi wote waliopo huko warudi nyumbani ili waishi maisha ya kawaida na watoto na ndugu zao. Kwa nini wengine wanaweza kutembea mitaani na wapendwa wao na wao hawawezi? Mbona hakuna anayewasaidia?", alihoji Maria Zimareva, ambaye kaka yake ni mmoja wa wapiganaji waliojichimbia kiwandani humo.

Naibu Waziri Mkuu Iryna Vereshchuk alikiambia kituo cha televisheni cha 1+1 kwamba mazungumzo yalikuwa yakiendelea kwa ajili ya kuwaondoa wapiganaji hao, kuanzia wale waliojeruhiwa vibaya zaidi.

Kisiwa cha Nyoka kilichoko bahari Nyeusi ambako mapigano yameshika kasi kati ya vikosi vya Ukraine na Urusi kuwania udhibiti wa pwani ya bahari Nyeusi. Ukraine imesema imeizamisha na kuitia moto meli ya kivita ya Urusi katika karibu na kisiwa hiki, Mei 12, 2022.Picha: AndreyxNekrasov/imagebroker/IMAGO

Mwanajeshi wa Urusi kushtakiwa kwa uhalifu wa kivita Kyiv

Mjini Kyiv, mahakama inatazamiwa hii leo kuanza kusikiliza kesi ya kwanza ya uhalifu wa kivita tangu vita kuanza mwezi Februari.

Soma pia: Ukraine inataka kuhakikishiwa nafasi Umoja wa Ulaya

Mwanajeshi wa Urusi anatarajiwa kufikishwa mahakamani akishtakiwa kwa mauaji ya raia huko Chupakhivka, kaskazini mashariki mwa Ukraine, Februari 28.

Na huko katika kisiwa cha Nyoka ambako mapigano makali yanaendelea kuwania udhibiti wa pwani ya Bahari Nyeusi, vikosi vya Ukraine vimesema vimeharibu meli ya ugavi ya Urusi karibu na kisiwa hicho na kisha kuitia moto.

Wakati mapigano yakiendelea kote nchini, mataifa yanalenga kumuongezea shinikizo Rais wa Urusi Vladimir Putin.

Soma pia: Ukraine: Zaidi ya wapiganaji 1,000 bado wamekwama Mariupol

Mawaziri wa mambo ya nje kutoka kundi la mataifa tajiri, G7, wanalenga kutoa kile Ujerumani ilichokiita "ishara yenye nguvu ya umoja" wanapokutana leo Ijumaa kujadili mzozo huo wanaohofia kuwa huenda ukasambaa hadi Moldova.

Ujerumani imesema inatafuta ishara imara ya umoja kwa ajili ya Ukraine wakati wa mkutano wa mawaziri wa mataifa yanayounda kundi la G7 mjini Berlin, Ijumaa, Mei 13, 2022.Picha: Kay Nietfeld/dpa/picture alliance

Mpango wa Finland kuomba uanachama wa NATO, uliotangazwa jana Alhamisi, na matarajio kwamba Sweden itafuata mkondo huo, italeta upanuzi wa muungano huo wa kijeshi wa Magharibi ambao Putin alilenga kuuzuia.

Ikulu ya Kremlin imeonya kuwa hatua ya mataifa hayo mawili kujiunga na NATO itajibiwa vikali.

Chanzo: Mashirika

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW